Kiba ajibu mapigo ya Diamond, Harmonize

BAADA ya Harmonize kusawazisha alichoanzishiwa Diamond Platnumz sasa ni zamu ya Alikiba kusepa na kofia ya Rais John Magufuli.

Sapraizi hiyo ambayo Alikiba amekutana nayo ni kuvishwa kofia na mgombea Urais kwa tiketi ya CCM, John Magufuli akiwa mkoani Kagera.

Kiba alipanda jukwaani na kutumbuiza kwa wimbo wa ‘Seduce me’, mara baada ya kumaliza aliimba wimbo wa Kidogo.

Wakati anashuka kuwafuata wananchi waliokuwa nyuma ya uzio, Alikiba aliitwa jukwaa kuu alilokaa Rais Magufuli, na Katibu wa Itikadi na Uenezi Taifa (CCM), Humphrey Polepole.

Alikiba akiwa anapanda katika jukwaa kuu alivuliwa kofia yake na mmoja ya walinzi kisha, alikwenda kukutana na Magufuli ambaye alivua kofia yake na kumvalisha msanii huyo.

Magufuli baada ya kumvalisha kofia Alikiba walianza kucheza wote kwa sekunde chache kabla ya msanii huyo kushuka jukwaani hapo na kuendelea kutumbuiza.

Alikiba anakuwa msanii wa tatu kuvalishwa kofia na Magufuli kwani hapo awali alianza, Diamond Platnumz kisha akafuata Harmonize.