Mwijaku kusomewa hoja za awali Oktoba 19

Upelelezi wa kesi ya kusambaza picha za utupu inayomkabili, mtangazaji wa Clouds, Mwemba Burton(35),maarufu kama Mwijaku, umekamilika.

Mwijaku, ambaye ni mkazi wa Mbezi Beach, anakabiliwa na shtaka moja la kusambaza picha za utupu kinyume cha sheria.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeelezwa hayo jana na upande wa mashtaka, wakati shauri hilo lilipowasilishwa mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa.

Wakili wa Serikali, Yusuph Abood aliieleza mahakama mbele Hakimu Mkazi Mkuu, Richard Kabate, kuwa upelelezi wa shauri umekamilika hivyo wanaomba tarehe nyingine kwa ajili kumsomea mshtakiwa hoja za awali(PH).

Hakimu Kabate, baada ya kusikikiza maelezo ya upande wa mashtaka, aliahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 19 mwaka huu, ambapo mshtakiwa atasomewa hoja za awali.

Mwinjaku yupo nje kwa dhamana, baada ya kukamilisha masharti ya dhamana katika kesi hiyo ya msingi ya jinai namba 110/2020.

Mshtakiwa anadaiwa kutenda kosa hilo, kati ya Septemba 17, 2019 na Oktoba 2019 katika jiji la Dar es salaam.

Katika kipindi hicho, Mwijaku anadaiwa kuchapisha picha za ngono kupitia mtandao wa kijamii wa WhatsApp uliounganishwa katika Kompyuta.

Mshtakiwa huyo anadaiwa kusambaza picha hizo, wakati akijua kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.