Wasanii kibao kupanda jukwaa moja Mwanza

KESHOKUTWA Ijumaa Septemba, 18, 2020 wakazi wa Jiji la Mwanza watashuhudia bonge la burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali katika tamasha la Pisi Kali litakalofanyika kwenye ukumbi wa Bundesliga.

Tamasha hilo ambalo litakutanisha wasanii wengi katika jukwaa moja, huenda likawa la kwanza jijini hapa tangu kuruhusiwa kwa shughuli mbalimbali za mikusanyiko baada ya kupungua kwa virusi vya corona ambavyo viliisumbua dunia.

Akizungumza na Mwanaspoti Online leo Jumatano Septemba 16, 2020, Mratibu wa tamasha hili, Mzee Mandawa amesema lengo ni kuwakutanisha wasanii chipukizi na wazoefu ili kujengeana uwezo lakini kubwa zaidi ni kuwapa burudani wakazi wa Mwanza.

Amewataja baadhi ya wasanii watakaopanda jukwaani kutoa burudani kuwa ni Awadh Chami ‘Morn Central Zone’, Laurent John ‘Law wa John’ na Hafidh Hassan ‘Holiday’ na kwamba kiingilio kitakuwa ni Sh 10, 000.

“Kimsingi ni kuwarudisha kwenye hali ya uchangamfu wadau wa burudani baada ya ugonjwa wa Covid 19 kupungua, niwaombe wakazi wa Mwanza kujitokeza kwa wingi katika tamasha hili” amesema Mandawa.

Kwa upande msanii, Law wa John amesema wamejipanga kutoa burudani nzuri kwa mashabiki wao na kwamba atatumia nafasi hiyo kutambulisha wimbo wake mpya uitwao Umarioo.

“Tangu kuingia kwa ugonjwa Covid 19, Mwanza ilikuwa imelala, kwahiyo kupungua kwa virusi hivyo, tutatoa shoo kali na kutambulisha kazi zetu mpya, naamini hawatajutia ujio wao” amesema msanii huyo.

Naye Holiday amesisitiza kuwa ikiwa n imara yake ya kwanza kupata nafasi ya kusimama jukwaani na wasanii wakubwa, ataonesha uwezo wake kwenye kazi yake hiyo ya muziki.