Zuchu Nandy kuchuana tuzo za AFRIMMA

Muktasari:

Msanii huyo ambaye ni mtoto wa malkia wa nyimbo za taarabu nchini Tanzania, Hadija Kopa  alitangazwa kujiunga rasmi na lebo ya WCB, Aprili 8,2019 na tayari ameshaachia EP yake yenye nyimbo nane.


Hatimaye mtandao wa tuzo za African Muziki Magazine Award (AFRIMMA), zimetoa majina ya wateule watakaowania tuzo hizo kwa mwaka 2020, huku msaniichipukizi Zuchu Othuman maarufu 'Zuchu' akiwa miongoni mwa wanaowania tuzo hizo.

Zuchu ambaye ana miezi minne tangu atambulishwe kwenye soko la muziki akiwa chini ya lebo ya WCB, inayomilikiwa na msanii Diamond Platnumz, katika tuzo hizo atachuana na wasanii wengine kutoka nchi za Afrika wakiwemo wa Tanzania Nandy na Maua Sama.

Msanii huyo ambaye ni mtoto wa malkia wa nyimbo za taarabu nchini Tanzania, Hadija Kopa  alitangazwa kujiunga na WCB, Aprili 8,2020 na tayari ameshaachia EP yake yenye nyimbo nane ambazo zinafanya vizuri kwa sasa

Nyimbo hizo ni pamoja na Nisamehe, Wana, Raha, Kwaru, Hakuna Kulala, Shindua, Mauzauza na Ashua aliyomshirikisha Mbosso.

Katika tuzo hizo za AFRIMMA, Zuchu kaingia katika vipengele viwili ikiwemo msanii bora wa kike nchi za Afrika Mashariki na msanii bora chipukizi Afrika.

Katika kipengele cha msanii bora wa kike Afrika Mashariki, Zuchu anachuana na Maua Sama, Rosa Ree na  Nandy wote kutoka  Tanzania.

Wengine waliopo katika kipengele hicho ni Tanasha Donna , Nadia Mukami, Akothee,Fena Gitu (FenaMenal) kutoka Kenya na Vimka Sheebah Karungi wa Uganda.

Katika kipengele cha msanii bora chipukizi, Zuchu atachuana na Kofi Mole na J Derobie(Ghana), Omah Lay na Oxlade(Nigeria),Fanicko(Benin),Shasha(Zimbabwe),Mc One (Cote d’ivoire),Edgar Domingos(Angola) na  Ami Faku wa Afika Kusini.

Wasanii wengine kutoka Tanzania kwa upande wa wanaume walioingia katika tuzo hizo ni Diamond Platnumz, Mbosso, Rayvany,AliKiba, Harmonize na muongozaji maarufu wa video za wasanii wa WCB, Kenny.