Barca kupiga mnada kibao

BARCELONA, HISPANIA. BARCELONA imeamua kuweka hadharani orodha ya mastaa 12 watakaopigwa bei kwenye dirisha hili la uhamisho wa majira ya kiangazi huku ikiwahusisha Luis Suarez, Martin Braithwaite na beki wa kati Samuel Umtiti.

Kocha mpya Mdachi Ronald Koeman amepanga kusafisha kikosi hicho ili kuleta mastaa wengine wapya watakaokuwa na uwezo wa kuipeleka kwenye hatua ya juu zaidi Barcelona.

Jambo hilo limekuja muda mfupi baada ya Lionel Messi, aliyetishia kuhama timu hiyo kutengua mawazo yake na kutaka kubaki Nou Camp.

Mabosi wa Barcelona wanafahamu wazi kwamba kikosi chao kinahitaji marekebisho makubwa ikiwamo ya kuondoa baadhi ya mastaa na kuleta wachezaji wengine wapya.

Miamba hiyo ya Nou Camp ilikumbana na aibu kubwa baada ya kuchapwa 8-2 na Bayern Munich kwenye robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya mwaka huu.

Kipigo hicho kiliondoka na ajira ya kocha Quique Setien na hivyo nafasi yake kuzibwa na Koeman.

Wachezaji wengine wanaotajwa kwenye orodha hiyo ni Jean-Clair Todibo, Nelson Semedo, Arturo Vidal na Rafinha.

Pia wapo mastaa Monchu, Moussa Wague na Sergio Busquets. Barcelona inahaha kuunda upya kikosi chake katika dirisha hili la usajili.