Cheka aomba wakarudiane Malawi

Morogoro. Bingwa wa Dunia mkanda wa (WBO) mtanzania, Cosmas Cheka kutoka Morogoro amemweleza mpinzani mmalawi, Hannock Phiri kuwa kama hajaridhishwa na matokeo ya mchezo wao wa kuwania mkanda huo yeye yupo tayari kurudiana naye.

Cheka alisema kuwa katika pambano lao lililofanyika mwishoni mwa wiki na yeye kushinda kwa njia ya pointi lilikuwa kali na lenye upinzani mkali muda wote.

Cosmas alisema amemsikia mpinzani wake, Hannock Phiri akilalamika kuwa amependelewa na majaji katika ushindi wake jambo analipinga.

“Nimeshinda kihalali na haya malalamiko ya mpinzani wangu ni malalamiko ya kawaida hata mimi ningeshindwa ningelalamika lakini ndio mchezo ulivyo,”alisema Cosmas.

“Watu wanashindwa kuelewa, nimeanguka na kwenda chini lakini sio kuwa nimepigwa, bali nimempiga. Anacholalamika mpinzani wangu, Hannock Phiri anaona kama ameonewa, sio mbaya anaweza kutoa chalenji muda wowote tukarudiana hata huko kwao Malawi mimi niko tayari,” Cosmas.

Hatahivyo, wachambuzi wengi wa ngumi walikiri kwamba Cheka maji yalizidi unga kwenye pambano hilo.