Baraza kufyeka 10 Biashara Utd

KOCHA wa Biashara United, Francis Baraza
Muktasari:
- Baraza ameifanya Biashara United kuwa moja ya timu tishio kwenye Ligi Kuu kwani tangu aanze kuinoa timu hiyo Novemba mwaka jana ameiongoza katika michezo 19, ikishinda minane, ikitoka sare michezo minane na kipoteza mitatu dhidi ya Yanga, Simba na Lipuli.
KOCHA wa Biashara United, Francis Baraza amesema msimu ujao ataongeza wachezaji watano tu huku karibu wachezaji 10 wakitarajiwa kutemwa ndani ya kikosi hicho.
Baraza raia wa Kenya amesema anataka abaki na kikosi chenye wachezaji wachache ili aweze kukiongoza kwa ufanisi.
"Ukiangalia kwa sasa nina kikosi chenye wachezaji 31, ni wengi sana hivyo lazima msimu ujao wapungue kwani ukiwa na kundi kubwa hata kuliongoza kwa ufanisi ni kazi sana.
"Asilimia kubwa ya wachezaji wangu watabaki kwani natarajia kuongeza wachezaji watano tu ili kuongeza nguvu katika baadhi ya nafasi ambazo zimeonyesha mapungufu.
"Bado nina kikosi kizuri hivyo sitahitaji kukivuruga kwa kusajili wachezaji wengi msimu ujao, nataka kuwa na kikosi cha wachezaji 26 au 27 tu" amesema Baraza.
Wakati huo huo, Baraza amesema anaridhishwa na jinsi wachezaji wake wanavyofuata ratiba ya mazoezi aliowapa wakiwa nyumbani licha ya kwanza baadhi hawafanyi kwa asilimia 100.
" Nimekuwa nawafuatilia kupitia video na wengi wanajitahidi kuyafanyia kazi yake niliyowaelekeza na naamini ligi ikirejea hatutakuwa na shida sana"
"Tunatamani janga hili la virusi vya corona liishe ili ligi irejee na nilifurahi kuona Rais John Magufuli katika hotuba yake akiliongelea jambo hili hivyo naamini muda si mrefu ligi itarejea "amesema Baraza.
Biashara United inashika nafasi ya 10 kwenye msimamo wa Ligi ikiwa na point 40 baada ya kucheza michezo 29, imeshinda 10, imetoka sare michezo 10 na kupoteza tisa.