Mabeki wanaompa changamoto Fei Toto

Muktasari:

  • Fei Toto amewataja Ibrahim Abdullah 'Bacca' na Dickson Job kutoka Yanga kwamba wakikutana kwenye mechi anajua kazi siyo ndogo.

KIUNGO wa Azam FC, Feisal Sulum 'Fei Toto' amewataja mabeki wanaompa changamoto awapo uwanjani na kumfanya atumie akili nyingi kupenya katikati yao, akisema wawili wanatoka Yanga na mmoja anacheza naye timu moja.

Fei Toto amewataja Ibrahim Abdullah 'Bacca' na Dickson Job kutoka Yanga kwamba wakikutana kwenye mechi anajua kazi siyo ndogo.

"Kabla sijajiunga Azam nimecheza na Bacca na Job, nafahamu ubora wao kuanzia mazoezini na ndio maana namkumbali pia Abdallah Kheri 'Sebo', licha ya kucheza naye ananipa chalenji katika mazoezi," amesema na kuongeza;

"Sina maana kwamba Sebo ndiye bora peke yake Azam, bali ninapokutana na mabeki bora kwenye timu, wanakuwa wananiandaa kwa ajili ya ushindani halisi wa mechi za mashindano na nje ya Azam na Yanga kuna mabeki wengi wazuri hao ni baadhi tu."

Fei Toto ambaye anakimbizana kwenye ufungaji na winga wa Yanga, Stephane Aziz Ki, amelizungumzia hilo akiema halimpi presha, badala yake anafanya kazi kama inavyotakiwa.

Ki ana mabao 15 na Fei Toto 14 kwenye Ligi Kuu Bara, lakini Zanzibar Finest amesema hilo kwake siyo ishu: "Nafanya kazi zangu kwa bidii, ikitokea nikawa mfungaji bora ni sawa, kikubwa malengo ya timu kwanza."