Prime
Kivuli cha MK14 kinavyowatisha washambuliaji Ligi Kuu
MIONGONI mwa nyota wa kigeni waliofanya vizuri na kuweka rekodi bora katika Ligi Kuu Bara, hutoacha kumtaja mshambuliaji wa zamani wa Simba, Singida Big Stars na Namungo FC, Meddie Kagere ‘MK14’ kutokana na uwezo wake mkubwa aliokuwa nao.
Kagere aliyezaliwa Oktoba 10, 1986, Uganda akiitumikia timu ya taifa ya Rwanda ‘Amavubi’, ametimiza miaka 39, huku kwa mujibu wa wikipedia amecheza kwa miaka 21 tangu aanze kucheza soka 2004 akiwa na Mbale Heroes FC ya Uganda.
Nyota huyo aliyetamba na timu mbalimbali za Gor Mahia, ATRACO FC, Kiyovu Sports, Police FC na Rayon Sports akiwa Simba aliweka rekodi ya kipekee katika Ligi Kuu Bara ambayo hadi sasa imetimiza msimu wa sita bila ya kufikiwa wala kuvunjwa.
Mchezaji huyo raia wa Rwanda wakati anaondoka Msimbazi aliweka rekodi tamu kwa mastaa wa kigeni katika Ligi Kuu Bara ambayo imeendelea kuishi hadi leo, kwani licha ya wachezaji wengi waliokuwa bora na wazoefu kucheza ila wameshindwa kuifikia.
Kagere alitua Simba akitokea Gor Mahia ya Kenya msimu wa 2018-2019 na kufunga mabao 23 na kuipiku rekodi ya aliyekuwa mshambuliaji wa Yanga, Amissi Tambwe ya wachezaji wa kigeni kufunga mabao mengi msimu mmoja alipofunga 21 msimu wa 2015-2016.
Msimu wa pili kwa staa huyo akiwa na Simba pia, alifunga mabao 22 na kutetea tuzo ya mfungaji bora ikiwa pia ni rekodi kwani, haikuwahi kutokea kwa mchezaji yeyote iwe mzawa au wa kigeni kutwaa tuzo ya ufungaji bora mara mbili mfululizo.
Nyota wengine waliotwaa tuzo ya mfungaji bora japo kwa msimu tofauti tangu mwaka 2000 ni Simon Msuva, Amissi Tambwe na John Bocco.
Bocco alitwaa msimu wa 2011-2012 enzi akiwa na Azam FC alipofunga mabao 19 akairudia tena 2020-2021 alipokuwa na Simba akifunga 16 huku Tambwe akiichukua 2013-2014 na Simba alipofunga 19 kisha akaichukua alipokuwa Yanga 2015-2016 akifunga 21.
Kwa upande wa Simon Msuva alichukua tuzo hiyo akiwa na Yanga akifanya hivyo msimu wa 2014-2015 alipofunga mabao 17 kisha akairudia tena msimu wa 2016-2017, wakati alipofunga 14 sambamba na aliyekuwa nyota wa Ruvu Shooting, Abdulrahman Mussa.
Kwa ujumla tangu Kagere alipoanza kucheza Ligi Kuu Bara, amefunga jumla ya mabao 77, ambapo akiwa na Simba msimu wa 2018-2019, alifunga 23, 2019-2020, akafunga 22, 2020-2021 akatupia 13 kisha msimu wa mwisho wa 2021-2022, akaifungia saba.
Baada ya hapo nyota huyo akajiunga na Singida Big Stars ambapo msimu wake wa 2022-2023, alifunga mabao nane, huku 2023-2024, aliochezea Singida Fountain Gate, kisha dirisha dogo akajiunga na Namungo FC ‘Wauaji wa Kusini’, alifunga mawili.
Msimu wa mwisho kwa nyota huyo kucheza Ligi Kuu, ulikuwa ni wa 2024-2025, akiwa Namungo FC, aliyoachana nayo tangu Julai 1, 2025, aliyoifungia mabao mawili katika ushindi wa timu hiyo wa 5-0, dhidi ya KenGold ya jijini Mbeya, Juni 22, 2025.
Nyota huyo ametwaa jumla ya mataji tisa akiwa Simba, ambapo Ligi Kuu Bara amechukua mara tatu msimu wa 2018-2019, 2019-2020 na 2020-2021, huku Kombe la Shirikisho la FA (Sasa CRDB) amechukua mawili kuanzia msimu wa 2019-2020 na 2020-2021.
Mataji mengine aliyochukua mshambuliaji huyo ni Ngao ya Jamii aliyochukua mara tatu mwaka 2018, 2019 na 2020, huku Kombe la Mapinduzi ambalo ni taji lake la mwisho kuchukua akikichezea kikosi hicho cha Simba alilichukua mara moja mwaka 2022.
REKODI YA WALIOFUATA
Baada ya Kagere kuchukua tuzo ya mfungaji bora msimu wa 2018-2019 na 2019-2020, msimu wa 2020-2021 akaichukua aliyekuwa nahodha wa Simba, John Bocco anayeifundisha kwa sasa timu ya vijana ya kikosi hicho, aliyemaliza kwa kufunga mabao 16.
Bocco anashikilia rekodi ya kipekee ya mfungaji bora wa muda wote wa Ligi Kuu kwa kufunga mabao 156 akiifungia Azam FC mabao 84, baada ya mshambuliaji huyo kukitumikia kikosi hicho kwa misimu tisa kuanzia msimu wa 2008-2009 hadi 2016-2017.
Baada ya hapo akajiunga na Simba akiitumikia kwa misimu saba kuanzia msimu wa 2017-2018 hadi 2023-2024 akiifungia mabao 70, huku msimu wake wa mwisho kucheza ulikuwa wa 2024-2025 na kikosi cha JKT Tanzania alichokifungia mawili.
Mabao 156 ya Bocco yalivunja rekodi ya mfungaji bora wa muda wote katika Ligi Kuu iliyokuwa inashikiliwa na aliyekuwa nyota wa Bandari Mtwara, Yanga, Simba, Mmbanga na Twiga Sports, Mohamed Hussein ‘Mmachinga’ aliyefunga mabao yake 153.
Baada ya Bocco akafuatia aliyekuwa mshambuliaji wa Geita Gold, George Mpole aliyefunga mabao 17 kwa msimu wa 2021-2022 japo msimu wa 2022-2023 alishindwa kuonyesha makali na kushuhudia nyota huyo akimaliza na mabao mawili.
Msimu wa 2023-2024, Mpole hajafunga bao lolote la Ligi Kuu, ingawa Januari 1, 2023 alijiunga na FC Saint-Eloi Lupopo ya DR Congo kisha kurejea Bongo msimu wa 2024-2025 na kuifungia mabao mawili Pamba Jiji ‘TP Lindanda’ au ‘Wanakawekamo’.
Mpole aliyewahi kucheza Mbeya City na Real Nakonde ya Zambia, msimu wa 2025-2026, anacheza Tanzania Prisons aliyojiunga nayo dirisha dogo la Januari 2026 baada ya kutokuwa na timu, huku akiwa tayari ameifungia mabao manne ya Ligi Kuu Bara.
Msimu wa 2022-2023 tuzo hiyo ya mfungaji bora ilienda kwa nyota wawili ambao ni Fiston Mayele aliyekuwa Yanga na Saidi Ntibazonkiza ‘Saido’ aliyeanza na Geita Gold kisha Januari 2023 akajiunga na Simba, baada ya wote kufunga pia mabao 17.
Mayele alijiunga na Yanga Agosti 1, 2021 akitokea AS Vita Club ya kwao DR Congo, ingawa aliondoka pia Julai 30, 2023 na kujiunga na Pyramids FC ya Misri anayoendelea kuichezea hadi sasa akiwa ni miongoni mwa washambuliaji bora kwa Afrika.
Msimu wake wa mwisho alikuwa mfungaji bora na kuifikisha Yanga fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika msimu wa 2022-2023, japo ilikosa ubingwa kwa faida ya bao la ugenini, baada ya sare ya jumla ya mabao 2-2 dhidi ya USM Alger ya Algeria.
Pia, Ikumbukwe Mayele katika msimu wa 2022-2023, licha ya kuifikisha Yanga hadi fainali na kukosa taji hilo kubwa, lakini aliibuka mfungaji bora wa Kombe la Shirikisho Afrika, baada ya mshambuliaji huyo nyota kufunga mabao yake saba.
Kwa upande wa Saidi Ntibazonkiza ‘Saido’ aliyewahi kucheza pia Yanga aliyojiunga nayo mwaka 2020 akitokea Vital’O FC ya kwao Burundi, aliachana na Simba, Julai 1, 2024, huku akiwa ameifungia mabao 11, ya Ligi Kuu kwa msimu wa 2023-2024.
Msimu wa 2023-2024, Stephane Aziz KI akachukua tuzo ya mfungaji bora baada ya kuifungia Yanga mabao 21, ikiwa ni kiwango kizuri kwa kiungo huyo mshambuliaji, kilichowavutia mabosi wa Wydad Casablanca ya Morocco kumsajili Juni 1, 2025.
Aziz KI alijiunga rasmi na Yanga Julai 15, 2022, akitokea ASEC Mimosas ya Ivory Coast, ambapo licha ya kujiunga na Wydad ya Morocco ila aliachana nayo Januari 24, 2026, kisha kujiunga na Al-Ittihad SC ya Libya anayoendelea kucheza hadi sasa.
Msimu uliopita wa 2024-2025, aliyekuwa kiungo mshambuliaji wa Simba, Jean Charles Ahoua, akatwaa tuzo hiyo ya mfungaji bora, baada ya kufunga mabao 16 ya Ligi Kuu Bara, ikiwa ni msimu wake wa kwanza tu kwa nyota huyo ndani ya kikosi hicho.
Kwa msimu wa 2024-2025, Ahoua alichangia mabao 25 kati ya 69, ya Simba katika Ligi Kuu, baada ya kufunga 16 na kuasisti mengine tisa, huku akiiwezesha kumaliza ya pili na pointi 78, nyuma ya mabingwa watetezi Yanga iliyomaliza na pointi 82.
Msimu huu wa 2025-2026, kiungo huyo ameondoka akiwa amechangia mabao mawili ya Ligi Kuu Bara, baada ya kufunga moja na kuasisti moja, ambapo yote yalikuwa ni katika ushindi wa timu hiyo wa 3-0, dhidi ya Fountain Gate, Septemba 25, 2025.
Ahoua aliyejiunga na Simba Julai 3, 2024, akitokea Stella Club d’Adjame ya kwao Ivory Coast, alikuwa mchezaji bora wa Ligi Kuu ya Ivory Coast kwa msimu wa 2023-2024, baada ya kuhusika na mabao 21, akifunga 12 na kuchangia tisa (Assisti).
Nyota huyo aliyecheza LYS Sassandra na Sewe Sports kabla ya Stella, alijiunga na CR Belouizdad ya Algeria, Januari 22, 2026, baada ya kucheza Simba mwaka mmoja na nusu, licha ya kubakisha mkataba wa miezi sita uliokuwa uishe Juni 30, 2026.
Tangu msimu wa 2018-2019 na 2019-2020, Kagere alipoibuka mfungaji bora mara mbili mfululizo, hakuna mchezaji yeyote wa Ligi Kuu aliyefikia au kuivunja rekodi hiyo ikitimia kwa sasa msimu wa sita licha ya nyota mbalimbali bora wanaoonekana.