Hababuu Ali aendeleza moto wa KVZ
Muktasari:
- KVZ imefikisha pointi 55, kileleni baada ya kukusanya pointi sita katika michezo yake miwili iliyocheza kwenye Uwanja wa Gombani, Pemba na kufanikiwa kushinda 3-2 dhidi ya New Stone Town kabla ya kuichapa Fufuni 2-1.
KOCHA Mkuu wa KVZ, Hababuu Ali ameendeleza pale walipoishia watangulizi wake kwa kuiongoza timu hiyo kushinda mechi mbili na kuendelea kukaa kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu Zanzibar (ZPL).
KVZ imefikisha pointi 55, kileleni baada ya kukusanya pointi sita katika michezo yake miwili iliyocheza kwenye Uwanja wa Gombani, Pemba na kufanikiwa kushinda 3-2 dhidi ya New Stone Town kabla ya kuichapa Fufuni 2-1.
Ushindi huo unamfanya Hababuu aliyekabidhiwa kikosi hicho baada ya kuondoka kwa kocha Malale Hamsini na Ali Khalid Omar 'Kisoda', kuendelea kubaki kileleni.
KVZ imeendelea kusalia kileleni katika msimamo wa ligi ikiwa na alama 55 katika michezo 26 iliyocheza huku nafasi ya pili ikishikwa na JKU iliyokusanya pointi 49 ikiwa na michezo 25.
Kocha Hababuu aliyewahi kuinoa KMKM, amesema licha ya ushindi huo, kwa sasa timu hiyo inakabaliwa na vitu viwili vikubwa ikiwemo mpangilio wa ratiba iliopo na pamoja na ushindani mkali kutoka kwa wapinzani wake wanaowania nafasi hiyo.
Hababuu amesema, katika kipindi hiki kila mmoja anapambania nafasi yake kwani zipo ambazo zinahitaji ubingwa, nne bora na nyingine kulinda heshima zao.
Pia, amesema pointi sita zilizopatikana kisiwani Pemba ni njia nzuri ya kufikia malengo yao ya kubeba ubingwa msimu wa 2025-2026.
"Kiu ya KVZ ni ubingwa na sio kingine, hivyo hatutoacha kupambana kutimiza hilo na litafanikiwa," amesema.
Kocha Hababuu amesema, kinachompa morali na hamasa kwa timu hiyo ni kuona namna wachezaji wanavyopambana kila mechi kutaka matokeo mazuri.
Pia, amesema katika timu hiyo anakutana na vitu viwili ikiwemo kukosa muda wa kutosha wa kujiandaa na mechi kwani bado hajawazoea wachezaji na kingine ni timu kutaka ubingwa.
Amesema, ili kufanya vizuri lazima timu zijiandae kwa kupata muda wa kutosha kufanya hivyo kwa ajili ya kuhimili mapambano.
Naye, kipa na nahodha wa timu hiyo, Bashir Muslim Darueshi, amesema umoja na mshikamo ndiyo siri ya mafanikio yao katika michezo miwili ya ugenini kisiwani Pemba.
Kipa huyo amesema malengo yao yalikuwa ni kushinda michezo yote na wanashukuru wamefanikiwa baada ya kupambana.
Darueshi amesema ilikuwa si rahisi kushinda michezo hiyo kwani walikutana na ugumu kama si kupambana na kufuata maelekezo ya mwalimu wasingefanikiwa kushinda.