Mpole ndo basi tena Kagera Sugar

Muktasari:
- Kagera ilimsajili Mpole kupitia dirisha dogo msimu huu kwa mkopo akitokea Pamba Jiji ya Mwanza lakini mshambuliaji huyo ameshindwa kujiunga kwa wakati.
KAGERA Sugar imelifunga rasmi faili la kumshawishi mshambuliaji George Mpole kwa kile ilichodai haitaki kuharibu utulivu wa hesabu zao za kubaki Ligi kuu.
Kagera ilimsajili Mpole kupitia dirisha dogo msimu huu kwa mkopo akitokea Pamba Jiji ya Mwanza lakini mshambuliaji huyo ameshindwa kujiunga kwa wakati.
Taarifa zinasema Mpole ameshindwa kujiunga na Kagera kutokana na kilichoelezwa hawakufikia makubaliano mazuri.
Mpole inaelezwa aliwapa sharti Kagera kwamba atatua klabuni hapo mara tu atakapoingiziwa fedha walizokubaliana ili aende kufanya kazi. “Kweli tulikuwa tunamuhitaji lakini tumeona mambo yanakuwa mengi mara leo anataka hili, kesho mambo yanabadilika, umekuwa ni usumbufu mkubwa tumeamua kumuachia afanye maamuzi yake.
“Unaona hali ya nafasi tuliyopo kila mmoja anajikita kutafuta ni namna gani tutabaki Ligi Kuu na mechi ni ngumu, kwahiyo kuendelea kuhangaika na mchezaji mmoja hii nadhani sio sawasawa,” alisema bosi mmoja wa Kagera Sugar.
Hata hivyo, licha ya dili hilo kukwama, Mpole hajarudi Pamba Jiji.