Pointi moja yarejesha matumaini Malindi
Muktasari:
- Malindi iliipata pointi hiyo katika mechi ya raundi ya 24, Mei 4, 2026 kwenye Uwanja wa Mao, kisiwani Unguja, ikitoka sare ya 1-1 na Mafunzo.
POINTI moja iliyoipata Malindi katika Ligi Kuu Zanzibar, imefufua matumaini ya kubaki kwenye ligi hiyo licha ya kuwa katika mstari wa kushuka daraja.
Malindi iliipata pointi hiyo katika mechi ya raundi ya 24, Mei 4, 2026 kwenye Uwanja wa Mao, kisiwani Unguja, ikitoka sare ya 1-1 na Mafunzo.
Hadi kufikia sasa, timu mbili zinazotokea Pemba zimeshashuka daraja ambazo ni New Stone Town na Junguni United huku zikisubiriwa mbili kuungana nazo kukamilisha hesabu ya nne kwa mujibu wa kanuni za ligi hiyo.
Akizungumza na Mwanaspoti, Meneja wa Malindi, Ramadhan Sanga alisisitiza hawawezi kushuka daraja na wataonyesha maajabu yao katika mechi ijayo dhidi ya Mlandege, Mei 17, 2026.
Amesema pointi moja waliyoipata kwa Mafunzo, imewarejeshea imani kubwa wakifikisha pointi 25 baada ya mechi 24, zikibaki sita kumaliza msimu huu.
"Tulishazungumza, kila mechi iliyo mbele yetu ni kama fainali, tulikwenda kutafuta pointi tatu, lakini tumepata moja, tutakuwa bora zaidi mechi zijazo na tutawashangaza watu dhidi ya Mlandege," amesema.
Amesema viongozi pamoja na wachezaji watashirikiana kuhakikisha wanaibakisha timu hiyo Ligi Kuu na kuzima matarajio ya wengi wanaodai inashuka daraja msimu huu.