Yanga yatimba Azam FC kumng’oa Mtasingwa

Muktasari:

  • Mtasingwa ameonyesha kiwango bora miezi sita aliyocheza Ligi Kuu Bara akiitumikia Azam FC. Chanzo cha kuaminika kutoka Yanga kimeliambia Mwanaspoti kuwa wako kwenye mchakato wa kusaka kiungo mkabaji mwenye uwezo wa kuwapa changamoto waliopo.

KUNA kila dalili kiungo mkabaji wa Azam FC, Adolf Mtasingwa atasaini mkataba wa miaka miwili kuitumikia Yanga wikiendi hii.

Mtasingwa ameonyesha kiwango bora miezi sita aliyocheza Ligi Kuu Bara akiitumikia Azam FC. Chanzo cha kuaminika kutoka Yanga kimeliambia Mwanaspoti kuwa wako kwenye mchakato wa kusaka kiungo mkabaji mwenye uwezo wa kuwapa changamoto waliopo.

Mmoja wa viongozi wa Azam FC alisema Yanga huenda wakafanikiwa kwenye ushawishi wa fedha na mchezaji huyo kutaka changamoto mpya.

Mtasingwa bado ana mkataba wa miezi sita na Azam ambayo huenda akainunua na kusepa zake. Mwanaspoti lilifanya jitihada za kumtafuta Mtasingwa kujua hatma yake ndani ya Azam FC ambaye alikiri kuwa bado ni mchezaji wa Azam FC huku akisisitiza gazeti hili lisimnukuu kwa lolote kwani hataki kuchafua hali ya hewa.

“Bado unafuatilia hii stori mwanzo ulinitafuta nakumbuka nilikujibu kuwa mimi ni mchezaji wa Azam FC na kwenye hili aliyekupa taarifa ya mwanzo naomba umfuate akuthibitishie kama dili limekamilika,”alisema na kusisitiza yupo mapumzikoni.