Straika Kenya afariki dunia
Muktasari:
- Nyota huyo (31) alifariki baada ya kuugua kwa muda mrefu ugonjwa wa mishipa ya neva (Motor Neurone Disease, MND)
STRAIKA wa zamani wa AFC Leopards na timu ya taifa ya Kenya 'Harambee Starlets', Ezekiel Otuoma amefariki dunia usiku wa kuamkia leo baada ya kuugua kwa muda mrefu.
Nyota huyo (31) alifariki baada ya kuugua kwa muda mrefu ugonjwa wa mishipa ya neva (Motor Neurone Disease, MND)
Kupitia ukurasa wake wa Tiktok, Mke wa mchezaji huyo, Rachel Otuoma alithibitisha kifo cha mumewe kwa kuandika ujumbe wa majonzi.
"Kwa Mume wangu uliacha pengo moyoni mwangu ambalo hakuna mtu mwingine anaweza kujaza, mikono yangu iliyo tupu inanukia upendo tuliogawana upendo wako ulikuwa zawadi na nitauenzi milele," aliandika Rachel akiambatanisha na picha za Otouma.
"Ingawa ulikwenda mapema sana jambo hilo lilivunja moyo wangu uliaga siku ya kuzaliwa kwangu haitakuwa sawa tena hukuonyesha dalili yoyote au hata kusema neno la kuaga uliondoka bila kusema kwaheri katika maisha nilikupenda sana na hata baada ya kifo nakupenda zaidi," aliongeza.
Otuoma aligunduliwa kuwa na ugonjwa wa mishipa ya Neva mwaka 2020, hali ambayo iliathiri afya yake na kumfanya astaafu soka.
Ugonjwa huo, unaojulikana pia kama Amyotrophic Lateral Sclerosis (ALS), hushambulia Neva za miguu katika ubongo na uti wa mgongo, na kusababisha kudhoofika kwa misuli na kupoteza uwezo wa kufanya kazi za msingi za mwili.
Tangu kipindi hicho Otuoma alipoteza uwezo wa kutembea na hata kuzungumza, hali iliyomlazimu kumtegemea mke wake Rachel.
Otuoma alichezea baadhi ya timu nchini Kenya, ikiwemo AFC Leopards, Ulinzi Stars, na FC Talanta.