Dabi ya Kariakoo kupigwa Isamuhyo Mei 3
Muktasari:
- Uwanja huo ambao ndiyo unatumiwa na miamba hiyo, umepata baraka ziote za Bodi ya Ligi Kuu Bara baada ya awali mechi hiyo kupangwa kufanyika kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa.
BAADA ya kitendawili cha wapi mechi ya Kariakoo Derby itapigwa. Hatimaye majibu yamepatikana na Simba imetangaza itaikaribisha Yanga kwenye Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Mei 3.
Uwanja huo ambao ndiyo unatumiwa na miamba hiyo, umepata baraka ziote za Bodi ya Ligi Kuu Bara baada ya awali mechi hiyo kupangwa kufanyika kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Awali Simba ilituma maombi ya kutaka kuutumia Benjamin Mkapa kabla ya kutoka taarifa ya zuio la kuutumia lililotolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa na kwa sasa unaendelea kufanyiwa maboresho.
Ikumbukwe baada ya mechi ya Azam na Yanga iliyochezwa Machi 15, 2026 Msigwa alitoa taarifa rasmi uwanja huo umefungwa kupisha maboresho.
Meneja wa uwanja huo, Gabriel Mwasele alikiri maboresho hayo yanaendelea ila eneo la kuchezea bado halijaguswa, jambo ambalo liliongeza ugumu zaidi kwa Simba kupata nafasi hapo.
ZANZIBAR NOMA
Katika baadhi ya mechi ambazo Simba ilitumia Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar, haikupata matokeo mazuri na awali ilidhaniwa miamba hiyo ingeenda kukipiga visiwani huku kutokana na ubora wa uwanja huo na kwa kuwa zote zipo huko kushiriki Kombe la Muungano.
Mkosi huo wa kutokupata matokeo ikiwamo mechi za kimataifa za Caf na ilipokutana na Yanga na kusuluhu, zinaweza kuwa ni moja ya sababu ya kuwarudisha Isamuhyo baada ya kuukosa Kwa Mkapa.
WASIKIE BODI
Kupitia taarifa iliyotolewa na Bodi ya Ligi Kuu ilitangaza mabadiliko ya uwanja wa mchezo namba 169 msimu 2025/26 kati ya Simba na Yanga.
“Mchezo huo ambao hapo awali ulipangwa kufanyika kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa, sasa utachezwa Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Mei 3. kuanzia saa 12:00 jioni,” ilisema taarifa hiyo na kuongeza,
“Sababu za mabadiliko hayo ni Uwanja wa Benjamin Mkapa kuwa kwenye matengenezo.”
“Klabu za Simba na Yanga pamoja na wadau wengine wa Ligi Kuu Bara wamepatiwa taarifa zote kuhusiana na mabadiliko ya uwanja wa mchezo huo na maandalizi yake yanaanza mara moja ili kuhakikisha unafanyika katika kiwango cha juu kinachoendana na hadhi ya michezo mikubwa ya ligi ya sita kwa ubora Barani Afrika.
PATATOSHA?
Kutokana na ukubwa wa mechi hiyo maswali ya wengi ni kama uwanja huo utaweza kuhimili mechi kubwa kama Derby ambayo inachezwa hapo kwa mara ya kwanza, huku uwanja huo ukiwa na uwezo wa kuchukua mashabiki 5000 tu.