Hausung yamkomalia Pacome

TUTASHANGAZA. Ni kauli iliyoitoa Hausung FC wakati ikijiandaa na mchezo wao wa Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) dhidi ya Yanga unaotarajia kupigwa kesho Jumanne kwenye Uwanja wa Azam Complex Chamazi.

Timu hiyo ambao ni mabingwa wa Mkoa wa Njombe, inatarajia kucheza na Yanga ikiwa ni mara ya kwanza kukutana na vigogo hao wa soka nchini.

Akizungumza na Mwanaspoti, kipa wa timu hiyo, Alex Kifanyi alisema pamoja na ubora, uwezo na uzoefu ilionao Yanga lakini hawataingia kinyonge uwanjani.

Kipa huyo alisema Yanga sio ya kukaba mchezaji mmoja isipokuwa yoyote anaweza kuleta madhara kama hawatakuwa makini huku akieleza watamchunga zaidi, Pacome Zouzoua aliyekuwa kwenye kiwango bora tangu ajiunge nao akitoka ASEC Mimosas ya kwao Ivory Coast.

“Hata sisi msituchukulie poa, tumekuwa na muda mzuri wa kujiandaa hivyo tunaitaka hiyo mechi, tutashangaza mashabiki wengi, tunaiheshimu Yanga ila siyo kuwaogopa, tutakuwa makini na mchezaji yeyote ila zaidi Pacome,” alisema kipa huyo.

Kwa upande wa kocha mkuu wa timu hiyo, Shangwe Michael alisema licha ya ratiba kuja ghafla ila waliisubiri mechi hiyo kwa hamu.

“Vijana morali yao ni ileile japokuwa ratiba imekuja kwa kushtukiza, tunaenda kuonyesha uwezo wetu na ninaamini historia itaandikwa.”

Mbali na mechi hiyo ya Yanga na Hausung, kesho pia kuna michezo miwili ya viporo vya hatua ya 16 Bora ya ASFC ambapo Mtibwa Sugar itacheza na Nyakagwe ya Geita na Kagera Sugar itakayoumana na Dar City kabla ya keshokutwa Jumatano, Simba kuvaana na Tembo Fc ya Tabora.