Kocha Pamba Jiji alia na mabeki
Muktasari:
- Pamba Jiji iliyoanza Ligi Kuu kwa kasi, hali imeonekana kubadilika kutokana na matokeo yasiyoridhisha katika michezo sita mfululizo bila ushindi.
MABAO sita waliyoruhusu Pamba Jiji katika mechi tatu mfululizo, yameonekana kumuumiza kichwa kocha mkuu wa timu hiyo, Francis Baraza akiwageukia mabeki akitaka kubadilika, huku akiwanyooshea pia vidole mastraika wake.
Pamba Jiji iliyoanza Ligi Kuu kwa kasi, hali imeonekana kubadilika kutokana na matokeo yasiyoridhisha katika michezo sita mfululizo bila ushindi.
Hata hivyo, mbali na ushindi, timu hiyo ya jijini Mwanza katika michezo hiyo sawa na dakika 540, imefunga mabao matatu, huku ikiruhusu manane na kushushwa hadi nafasi ya saba kwa pointi 26.
Katika mechi hizo, ilifungwa dhidi ya Yanga (3-0) na TRA United (1-0), huku ikitoa sare mbele ya Simba (1-1), Azam (2-2) na Mashujaa (0-0). Pia ilifungwa 2-0 na Coastal Union katika Kombe la Shirikisho la CRDB.
Akizungumza na Mwanaspoti, Baraza amesema wamepitia upepo mbaya na timu inatarajia kuendelea na mazoezi na ataanza kusuka upya nyota wake kurejesha makali.
“Ni sahihi katika michezo mitatu nyuma hatujafunga bao zaidi ya kuruhusu kwetu, nakubali matokeo na hali hii ya upepo mbaya imetupitia, lakini tunaweza kurekebisha kitu.
“Tunarejea mazoezini, naweza kusahihisha na kuimarisha maeneo hayo, nataka yale makali yarudi, beki isiruhusu bao lakini straika icheke na wavu, hii ndio falsafa yangu mpira wa kasi na mabao,” amesema kocha huyo.
Baraza raia wa Kenya aliyewahi kuinoa Biashara United, amekiri kwa sasa Ligi Kuu kuwa ngumu na yenye upinzani na bado hesabu zake ni kufukuzia nafasi nne za juu akitambia nyota wake kwamba wanaweza kufanya kitu.