Arne Slot akatisha likizo kisa Cherki

Muktasari:
- Kocha huyo raia wa Uholanzi alipata muda wa kupumzika baada ya msimu wa kwanza wa kuvutia akiwa Liverpool.
LIVERPOOL, ENGLAND: KOCHA wa Liverpool, Arne Slot ameripotiwa kukatisha likizo ili kukutana na Rayan Cherki kumshawishi atue Anfield.
Kocha huyo raia wa Uholanzi alipata muda wa kupumzika baada ya msimu wa kwanza wa kuvutia akiwa Liverpool.
Slot mwenye umri wa miaka 46 aliiongoza Liverpool kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu England ambalo ni la pili timu hiyo tangu 1992.
Liverpool tayari imeshakamilisha usajili wa Jeremie Frimpong kwa Pauni 29.5 milioni. Pia inakaribia kufanikisha dili la kihistoria la zaidi ya Pauni 109 milioni la staa wa Bayer Leverkusen, Florian Wirtz.
Hata hivyo, kwa kuwa dili la Wirtz bado halijakamilika mabingwa hao wa Ligi Kuu England wanaendelea kuangalia machaguo mengine mbadala. Na hilo linajumuisha mazungumzo na nyota wa Lyon, Cherki. Kwa mujibu wa The Athletic, Slot ambaye awali alionekana akifurahia mapumziko huko Ibiza, Hispania alikatisha likizo wiki iliyopita na kwenda Kusini mwa Ufaransa ambako alikutana na na Cherki kwa ajili ya mazungumzo.
Wirtz, mwenye umri wa miaka 22, ndiye chaguo kuu, lakini Cherki anasalia kuwa mbadala ikiwa mambo yatakuwa magumu.
Kama ilivyo kwa kiungo wa Bayer Leverkusen, Mfaransa huyo mwenye umri wa miaka 21 anaweza kucheza kama kiungo mshambuliaji au pembeni.
Hata hivyo, taarifa ya The Athletic inaonyesha Manchester City pia inavutiwa na Cherki, hasa baada ya kuachana na harakati za kumnasa Wirtz, huku wapinzani wao Manchester United nao wakionyesha nia.
Lyon ipo tayari kumwachia nyota huyo, lakini imepanga kupata ada kubwa ya uhamisho.