Maguire, Casemiro watikisa kimtindo
Muktasari:
- Kuna ofa kadhaa kutoka Saudi Pro League zinazomhusu Casemiro, wakati Maguire kuna timu za Ligi Kuu England ikiwamo West Ham United iliripotiwa kutaka saini yake. Lakini, wachezaji hao kuondoka kwenye dirisha la Januari hakuna kitu kama hicho na uwezekano ni mkubwa wakapewa dili mpya ili hata wakiuzwa, klabu ipate chochote kitu.
MANCHESTER, ENGLAND: NDO hivyo. Manchester United inaweza ikapata hasara ya kuwapoteza wachezaji wenye thamani ya Pauni 150 milioni bila ya kupata chochote wakati mikataba yao itakapofika tamati wakati wa dirisha lijalo la majira ya kiangazi.
Hata hivyo, bado kuna nafasi ya kuokoa walau pesa kidogo, endapo kama itaamua kuwapiga bei dirisha la Januari wachezaji hao ambao watakuwa huru mwisho wa msimu.
Wachezaji hao wenye thamani ya Pauni 150 milioni, yumo beki wa kati, aliyenaswa kwa Pauni 80 milioni, Harry Maguire na kiungo aliyesajiliwa kwa Pauni 60 milioni, Casemiro.
Beki wa kushoto, Tyrell Malacia aliyesajiliwa kwa Pauni 13 milioni na kipa Tom Heaton, ambaye hakuwa ameigharimu ada yoyote ya uhamisho Man United.
Wakati Heaton akitarajiwa kustaafu mwishoni mwa msimu, Malacia, ambaye bado hajacheza mechi yoyote msimu huu kwenye kikosi cha Man United baada ya kushindwa kuondoka kwenye timu hiyo dirisha lililopita, huenda akaondoka Januari au Juni.
Maguire na Casemiro wamekuwa wachezaji muhimu kwenye kikosi cha Ruben Amorim. Maguire amefunga mabao muhimu kwa timu hiyo chini ya Amorim, huku Casemiro akiwa nguzo imara kwenye safu ya kiungo ya miamba hiyo ya Old Trafford.
Maguire ana wasiwasi huenda huu ukawa msimu wake wa mwisho kwenye kikosi cha Man United kama hakutakuwa na dili lolote jipya mezani. Na kuhusu Casemiro, staa huyo huenda akalazimika kupunguza mshahara wake ili kubaki kwenye timu hiyo.
Kwenye kikosi cha Man United, wachezaji ambao wanaweza kuuzwa Januari ni Joshua Zirkzee na Kobbie Mainoo, lakini kwa Maguire, Casemiro, Malacia na Heaton kuna hatari kwa wachezaji hao wanne wakabaki hadi mwisho wa msimu na kuondoka bure kabisa.
Kuna ofa kadhaa kutoka Saudi Pro League zinazomhusu Casemiro, wakati Maguire kuna timu za Ligi Kuu England ikiwamo West Ham United iliripotiwa kutaka saini yake. Lakini, wachezaji hao kuondoka kwenye dirisha la Januari hakuna kitu kama hicho na uwezekano ni mkubwa wakapewa dili mpya ili hata wakiuzwa, klabu ipate chochote kitu.