Dakika 360 zaitega Malindi
Muktasari:
- Timu hiyo kwa sasa inapumulia gesi baada kupoteza mchezo mmoja kati ya mechi tano ambazo ilikuwa ni miongoni mwa matumaini yao makubwa katika harakati za kujinasua na janga la kushuka daraja.
DAKIKA 360 zilizosalia sawa na mechi nne za Ligi Kuu Zanzibar(ZPL), ndiyo itakayoamua hatma ya mabingwa wa zamani ZPL, Malindi kubaki katika ligi hiyo au kushuka daraja.
Timu hiyo kwa sasa inapumulia gesi baada kupoteza mchezo mmoja kati ya mechi tano ambazo ilikuwa ni miongoni mwa matumaini yao makubwa katika harakati za kujinasua na janga la kushuka daraja.
Hali si shwari kwa Malindi inayahitaji kushinda mechi zote nne zilizobaki ili kupata pointi 12 wakijumlisha na 25 walizonazo sasa zitawafanya kufikisha 37, huku ikiziombea mabaya Polisi, New King na Chipukizi zilizopo juu yake zipoteze.
Safari hiyo ya matumaini ya Malindi inategemea kupitia katika njia ngumu mbele ya Zimamoto, New King, Kipanga na Muembe Makumbi ambazo kila moja moja inamalengo yake kuelekea mwisho wa msimu huu.
Malindi itakuwa na kibarua kigumu kukabiliana na Zimamoto na Kipanga ambazo zipo katika vita ya kuwania kumaliza nne bora.
Kwa sasa Zimamoto ipo nafasi tano ikikusanya pointi 44 wakati Kipanga ikiwa nafasi ya saba na pointi 40.
Timu ya Muembe Makumbi ipo nafasi 11 na New King nafasi ya 12, zote zinapambana kujinusuru na hatari ya kushuka daraja, hivyo mechi hizo hazitakuwa rahisi.
Kwa sasa Malindi ipo nafasi ya 14 katika mstari wa kushuka daraja huku mbili za chini yake New Stone Town na Junguni United tayari zimeshashuka daraja ambapo zinatakiwa zingine mbili kukamilisha idadi ya timu nne zinazotakiwa kushuka.