DAKIKA ZA JIOOONI: Coastal Union na mwendelezo mbaya Ligi Kuu

Muktasari:
- Moja ya mafanikio yake makubwa ni kushinda Kombe la Nyerere mwaka 1980 na mwaka 1988 ilichukua kombe la ligi na mwaka 1989 ilipata nafasi ya kushiriki kombe la Washindi Afrika ila ilitolewa raundi ya kwanza.
Coastal Union ni moja ya klabu zenye historia katika soka la Tanzania na imeshiriki Ligi Kuu Bara kwa vipindi tofauti.
Moja ya mafanikio yake makubwa ni kushinda Kombe la Nyerere mwaka 1980 na mwaka 1988 ilichukua kombe la ligi na mwaka 1989 ilipata nafasi ya kushiriki kombe la Washindi Afrika ila ilitolewa raundi ya kwanza.
Pia imekuwa ikitoa wachezaji waliowahi kuitumikia timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars na wengine kuzitumikia timu kubwa za Simba na Yanga.
Nyota kama Bakari Mwamnyeto (Yanga) aliitumikia Coastal msimu 2018/2020 na mwaka 2020 akajiunga na Yanga mwaka huohuo beki mwenzie wa kati Ibrahim Ame (Mashujaa) akatimkia Simba.
Wengine ni Abdi Banda (Dodoma Jiji) aliichezea Coastal kati ya 2012 na 2014, kisha akajiunga na Simba mwaka 2014 Haruna Moshi alipita kikosini hapo 2013, kisha akaitumikia Simba mwaka 2015 na walikuwa nyota muhimu kwenye kikosi cha Stars.
Hata hivyo, msimu huu umekuwa na changamoto kubwa kwa timu hiyo ikijikuta katika nafasi za mkiani mwa msimamo wa ligi, jambo linaloweka hatari ya kushuka daraja.
Kwa sasa, Coastal Union inakabiliwa na mtihani mzito wa kupambana kusalia Ligi Kuu, ikihitaji kupata matokeo mazuri katika mechi zilizosalia ili kujinusuru na kushuka daraja kwenda Championship.
Ukosefu wa matokeo mazuri, mabadiliko ya benchi la ufundi mara kwa mara na uwezo mdogo wa kiuchumi ni miongoni mwa sababu zinazoifanya timu hiyo kutofanya vizuri.

MSIMU ULIOPITA
Kama kuna msimu bora kwa Coastal basi ni ule uliopita 2023-2024, timu hiyo ilipomaliza nafasi ya nne na pointi 43, baada ya kushinda michezo 11, sare 10 na kupoteza tisa, huku safu ya ushambuliaji ikifunga jumla ya mabao 22 na kuruhusu 19.
Nidhamu nzuri ya kuzuia kwa maana ya kuruhusu mabao machache iliisaidia kumaliza nafasi hiyo ambayo pia ilikuwa inawaniwa na Singida Black Stars.
Msimu huo Coastal ilifuzu michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika kwa mara ya kwanza tangu mara yake ya mwisho iliposhiriki kimataifa mwaka 1989.
Hata hivyo, ni kama bahati haikuwa upande wao na ikaishia hatua za awali ikitolewa na Bravos do Maquis ya Angola kwa jumla ya mabao 3-0.
Licha ya mafanikio hayo ila kikosi hicho kiliachana na aliyekuwa kocha mkuu David Ouma, Agosti 24, 2024, kwa kile kilichoelezwa na viongozi kutoridhishwa na mwenendo wa matokeo.
Ouma alijiunga na Coastal Union Novemba 9, 2023 akichukua nafasi ya Mwinyi Zahera anayefundisha Pamba Jiji, akizifundisha Sofapaka, Mathare United na Posta Rangers.
Kocha huyo aliyetawala soka la Kenya kwa zaidi ya miaka 21, akiwa na leseni ya UEFA, CAF A na uzoefu kutoka kituo cha michezo cha Ajax Amsterdam cha Uholanzi, amewahi pia kufundisha timu ya taifa ya Kenya ‘Harambee Stars’ chini ya Bobby Williams.

MSIMU HUU
Msimu huu timu hiyo haijaanza vyema ligi na kwenye mechi 24 imeshinda tano, sare 10 na kupoteza tisa ikiwa nafasi ya 12 kwenye msimamo wa ligi na pointi 25.
Kwa nafasi iliyopo Coastal sasa, ni wazi haijawa na muendelezo wa ilichokifanya msimu uliopita baada ya kuanza mmsimu vibaya.
Coastal imepishana pointi moja na Namungo iliyopo nafasi ya 13 ikiwa nazo 24 na kama itamaliza nafasi hiyo katika mechi sita zilizosalia, italazimika kucheza Play-off mwisho wa msimu ili kuendelea kusalia Ligi Kuu.
Oktoba 23, 2024, Coastal Union ilimtangaza aliyekuwa Kocha Mkuu wa Mbeya City, Yanga, Ihefu na Singida United, Juma Mwambusi kuchukua mikoba ya Ouma kwa mkataba wa mwaka mmoja.
Tangu Juma Mwambusi aiongoze timu hiyo amesimamia mechi 15 kati ya 24, ushindi mbili, sare nane na kupoteza mechi tano.
Coastal 0-1Yanga
Singida Black Stars 0-0 Coastal
KenGold 1-1 Coastal
Coastal Union 2-1 Prisons
Singida Fountain Gate 3-2 Coastal
Tabora United 1-1 Coastal Union
Coastal Union 1-1 KMC
Coastal Union 2-1 JKT Tanzania
Mashujaa 0-0 Coastal Union
Pamba 2-0 Coastal Union
Coastal Union 0-0 Azam
Namungo 0-0 Coastal Union
Coastal Union 0-3 Simba
Dodoma 0-0 Coastal Union
Kagera 2-1 Coastal.

MTIHANI ULIOPO
Mtihani uliopo kwa Coastal ni kusalia Ligi Kuu lakini ni kama takwimu zinawatupa mkono kwa kile kinachoendelea kukipata kwenye michezo hiyo.
Timu hiyo ni kama inaendeleza pale ilipoishia misimu mitatu nyuma na 2021-2022, ilimaliza nafasi ya saba na pointi 38, baada ya kushinda michezo 10 tu, sare minane na kupoteza 12, ikifunga jumla ya mabao 22 na kuruhusu 31.
Msimu uliofuatia wa 2022-2023 ikaepuka janga la kushuka daraja baada ya kucheza michezo 30, ikishinda minane, sare tisa na kupoteza 13, ikishika nafasi ya 12 na pointi 33, huku safu ya ushambuliaji ikifunga jumla ya mabao 25 na kuruhusu 35.

IMEFELI HAPA
Kitendo cha timu hiyo kuachana na Ouma ambaye alifanya vizuri ukiwa msimu wake wa kwanza uliiyumbisha kwa kiasi fulani Coastal ambayo ilikuwa na muendelezo wa kile walichokifanya.
Ni miongoni mwa makocha ambao walionekana kuleta manufaa kwenye kikosi hicho hasa kwenye eneo la kuzuia jambo ambalo wengine walishindwa kukifanya.
Timu hiyo ilifeli kumtimua Ouma kwa kosa la kufungwa mabao 3-0 na kiuhalisia Coastal ilikosa uzefu kwenye michuano hiyo ambayo ni mara ya pili kushiriki.
Ilipita takribani miaka 35 tangu Coastal ifuzu mwaka 1989 hivyo kwa kipigo kile ni wazi ilipaswa kujifunza na kuangalia namna nzuri ya kuiendea michezo hiyo ya kimataifa.
Mbali na kutimua kocha lakini kuondoka kwa kipa namba moja wa timu hiyo, Ley Matampi kiliathiri pia kwa kiasi fulani kwenye eneo la kipa.

ANAIBEBA COASTAL
Mshambuliaji Maabad Maulid Maabad ndiye nyota anayeonekana kuibeba timu hiyo kwa mabao matano aliyofunga msimu huu.
Nyota huyo alijiunga na kikosi hicho Julai 11, 2022 akitokea KVZ ya Zanzibar ambapo aliibuka mfungaji bora mara mbili mfululizo akianza msimu wa 2020/21 mabao 17, uliofuata 2021/22 alifunga 21.
Msimu wa kwanza 2022/23 alifunga manne na 2023/24 alifunga matatu.
MSIKIE KOCHA
Akizungumzia juu ya mipango ya kubaki Ligi Kuu msimu huu, Mwambusi alisema wana kazi ngumu kutokana kila timu inacheza kwa malengo lakini watapambana.
“Tunaheshimu timu zote kwani kila mpinzani lazima tumkabili, kwa sasa malengo ni kubaki kwenye ligi, tulipofikia hakuna kuonyesha mpira mzuri ni kwenda na mipango na kuondoka na pointi tatu,” alisema Mwambusi.
MECHI ZILIZOSALIA
April 10
Coastal Union v Singida Black Stars
April 21
Coastal Union v KenGold
Mei 12
Tanzania Prisons v Coastal Union
Mei 21
Coastal Union v Fountain Gate
Mei 25
Coastal Union v Tabora United
MSIKIE TITO
Akizungumzia juu ya kumaliza vibaya msimu huu, Meneja wa mashindano wa timu hiyo, Jonathan Tito alisema kucheza mbali na Tanga imekuwa sababu kubwa ya timu hiyo kufanya vibaya.
“Sababu kubwa ya sisi kuanza vibaya msimu huu hatukuwa na maandalizi mazuri mwanzoni, ukianza msimu mpya unapaswa kurekebisha mambo yaliyopita na kuanza upya hivyo hilo limesababisha kwa kiasi fulani,” alisema Tito na kuongeza;
“Nyingine hatukuchezea uwanja wetu wa nyumbani kwa maana ya Mkwakwani Tanga, tulianza kutumia viwanja vya KMC, Azam na baadae tukahamia Arusha hilo limetuathiri sana msimu huu.”