Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

VIWANGO: Ni majina tu ndio yatawabeba mastaa hawa kwenye klabu zao

Lionel Messi.

Muktasari:

  • Kama inavyotarajiwa, mamilioni ya pesa yatatumika katika  kutengeneza vikosi ambavyo vitakuwa na nguvu kubwa kwenye Ligi ya  Mabingwa Ulaya. Kutakuwa na pilikapilika nyingi kwenye kipindi hicho cha usajili.

LONDON, ENGLAND

UMEFIKA wakati wa klabu za Ulaya kupigana vikumbo kwenye  kusaka nyota wapya kwa ajili ya kuboresha vikosi vyao kabla ya msimu  mpya kuanza.

Kwenye mchakato huo wa kusaka nyota wapya, katika klabu hizo  lazima kutakuwapo na nyota watakaofunguliwa milango ya kutoka  kwenye klabu hizo.

Kama inavyotarajiwa, mamilioni ya pesa yatatumika katika  kutengeneza vikosi ambavyo vitakuwa na nguvu kubwa kwenye Ligi ya  Mabingwa Ulaya. Kutakuwa na pilikapilika nyingi kwenye kipindi hicho cha usajili.

Hata hivyo, kwenye mchakato huo kuna baadhi ya mastaa wenye  majina makubwa kwenye Ligi Kuu England watajiona kuwa wenye  furaha kwa kubaki kwenye klabu zao wanazochezea kwa sasa  utakapofika msimu ujao.

Wakati kikiwa kimefika kipindi cha klabu moja moja kujitathmini na  kujijenga upya, kuna wachezaji wachache watabaki kwenye timu zao  kwa sababu tu ya majina yao.

Eden Hazard

Si jambo jepesi kulumbana na Jose Mourinho kama mchezaji huyo na  kitu ambacho kimefanywa na Eden Hazard kinaweza kuwa mwanzo wa  klabu ya Chelsea kufeli kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Staa huyo wa Ubelgiji alifanya kosa kubwa kwa kukosoa mfumo wa  timu yake ya Chelsea ambao ndiyo umeifanya timu hiyo ifikie mahali  hapo ilipo. Hazard amemkosea adabu kocha wake na alistahili  kuadhibiwa.

Juan Mata anaweza kuwa shahidi mzuri kuwa Mourinho si kocha  mwoga wa kuwatupa kando wachezaji wake mastaa na jambo hilo  linaweza kumgharimu sana Hazard. Kwa sasa kumekuwa na ripoti  kwamba Chelsea inaweza kufikiria kumuuza mmoja kati ya mastaa wawili, Oscar na Hazard.

Kwa kile kilichotokea kwa sasa ni hadhi tu na jina ndicho kitu  kinachombakiza Hazard klabuni Chelsea kwa msimu ujao.

Karim Benzema

Kwa njia zipi Karim Benzema ataendelea kubaki kwenye kikosi bora  kabisa cha Real Madrid. Kucheza straika wa kati mbele ya mastaa  kama Gareth Bale, Cristiano Ronaldo, Luka Modric, Isco, Xabio  Alonso, Angel Di Maria na wengineo ungemtarajia Benzema awe tishio  zaidi kwenye kufunga.

Lakini, staa huyo wa Ufaransa ameshindwa kulifanya hilo na sasa Real  Madrid inafikiria mpango wa kumnasa Luis Suarez wa Liverpool.  Benzema ni straika mzuri, lakini tatizo lake amekuwa hana makali ya  kutisha zinapokuwa mechi kubwa. Benzema ni mara moja tu aliweza  kupitisha idadi ya mabao 20 kwenye Ligi Kuu Hispania na hali ilivyo  kwa sasa ni jina tu linakalomsaidia abaki klabuni hapo msimu ujao.

Shinji Kagawa

Bado hajaonyesha kiwango chake kilichotarajiwa na wengi ambacho  kiliishawishi Manchester United kutoa pesa kumsajili. Kiungo huyo  Mjapani, Shinji Kagawa, alishindwa kung’ara tangu timu hiyo  ilipokuwa chini ya kocha Alex Ferguson na hadi ilipokuwa na kocha  David Moyes.

Pengine kocha mpya atakayekuja klabuni hapo anaweza kuwa na  bahati na staa huyo na akapata muda wa kuonyesha makali yake kama  alivyokuwa kwenye kikosi cha Borussia Dortmund.

Franck Ribery

Kiti kimekuwa moto Allianz Arena kwa Pep Guardiola baada ya kikosi  cha Bayern Munich kukung’utwa na Real Madrid kwenye Ligi ya  Mabingwa Ulaya, lakini wachezaji wake mastaa wanastahili kubeba  lawama kwa matokeo hayo.

Winga Mfaransa Franck Ribery ni mmoja kati ya mastaa  waliomwangusha Guardiola. Ribery alikuwa na nafasi ya kumwenyesha  Cristiano Ronaldo kwamba ni yeye aliyestahili tuzo ya Ballon d’Or,  lakini matokeo yake alifunikwa vibaya na hakuonekana kuwa na kitu  chochote cha kufanya uwanjani.

Guardiola anaweza kufikiria kumpiga bei tu winga huyo na pesa  atakazopata akanunua wachezaji wengine ambao watakuwa na jipya la  kuifanyia timu. Ribery hana jipya analoweza kufanya Bayern kwa sasa  na kama ataendelea kubaki klabuni hapo hadi msimu ujao hilo  litatokana na jina lake tu.

Diego Costa

Kuna mtu mmoja alieleza kwanini Diego Costa, ameweza kufunga  zaidi ya mabao 10 katika msimu huu na kuwa mmoja wa mastraika  wanaowindwa duniani kwa sasa.

Chelsea inaonekana kushinda mbio za kumnasa staa huyo mwenye  umri wa miaka 25 anayekipiga kwenye kikosi cha Atletico Madrid na  kwamba klabu yake inasubiri kwa hamu sana pesa zitakazoletwa kwa  ajili ya mchezaji huyo.

Kwa ada ya zaidi ya Pauni 30 milioni ambazo zitawagharimu  watakaohitaji huduma ya mchezaji huyo, kocha Diego Simeone  atakuwa mwenye kukenua kwa bahati ya mchezaji huyo.

Ukweli Costa hana muda mwingi wa kuendelea kutamba na staa huyo  mzaliwa wa Brazil aliyechukua uraia wa Hispania ni aina ya mchezaji  wa msimu mmoja. Ametengeneza jina msimu huu na kupandisha  thamani yake, lakini zaidi ya hilo Costa atabebwa na jina lake.

Mesut Ozil

Mesut Ozil ni mfano mzuri wa wachezaji ambao wamekuwa  wakizidiwa na ada zao za uhamisho. Staa huyo aliyesainishwa kwa  pesa nyingi na Arsenal amekuwa na msimu mbaya, lakini watu bado  wanaitaka Arsenal izidi kusajili kwa pesa nyingi kitu ambacho  kimekuwa nadra sana kufanywa na klabu hiyo Ozil kwa kesi yake kwa sasa ni kwamba jina lake ndilo linalombeba  lakini si soka analocheza. Ni kitu kinachoeleweka wazi, kama Ozil  huyo sasa angeendelea kubaki Real Madrid isingekuwa rahisi kwake  kupata namba kwenye kikosi hicho. Pengine hata kwenye kikosi cha  Arsenal, anapangwa kutokana na jina lake au hadhi yake kwamba  alisajiliwa kwa pesa nyingi.

Robin van Persie

Straika Robin van Persie amekuwa kwenye wakati mgumu msimu huu  ambapo ameshindwa kufunga mabao na hata hali yake ya kiafya nayo  imekuwa utata mtupu. Ukweli ni kwamba hiki kilikuwa kipindi  mwafaka kwa Man United kupeana mkono wa kwaheri na staa huyo.

Ana umri wa miaka 30 na anasumbuliwa na tatizo la kuwa majeruhi  mfululizo, jambo hilo litamfanya staa huyo kuwa si mchezaji muhimu   kwenye kikosi hicho kwa msimu ujao zaidi ya kuwaongezea bili  kwenye mishahara tu.

Wakati klabu hiyo ikipanga kufanya mabadiliko, Van Persie haonekani  kuwa sehemu ya mipango hiyo na kwamba kitakachomfanya aendelee  kubaki Old Trafford msimu ujao ni jina lake na uswahiba na kocha  Louis van Gaal kama atakabidhiwa kuinoa timu hiyo.

Juan Mata

Kocha, David Moyes, amebeba lawama kwamba hakustahili kutumia  pesa nyingi kwenye kuinasa saini ya Juan Mata. Mengi yanasemwa   kwamba Man United imesajili mchezaji aliyekuwa akisugua benchi  Chelsea na tangu atue kwenye klabu hiyo amekuwa tofauti.

Mata amefunga mabao matano tangu atue Man United Januari mwaka  huu, lakini wachambuzi wa soka wanaamini usajili huo ulifanywa kwa  kuhamaki baada ya mambo kwenda kombo. 

Kitu ambacho Man United itakitaka kwa sasa ni wachezaji wanaotumia  nguvu na kasi ya kuwarudisha katika hadhi yao, lakini Mata si mchezaji  wa aina hiyo.

Lionel Messi

Staa wa Barcelona, Lionel Messi ni mwanasoka mahiri kwenye sayari  hii, lakini msimu huu kiwango chake kimeshuka. Japo kwamba si kitu  kinachopaswa kufanywa kwa haraka katika kumkosoa staa huyo, lakini  dalili zimeonekana kwamba mchezaji huyo ameanza kupungua kasi  yake ya awali hasa kutokana na sasa kusumbuliwa na hali ya kuwa   majeruhi mara kwa mara.

Klabu yake ya Barcelona kwa sasa inamtazama Mbrazili Neymar kama  mtu atakayeweza kuipandisha tena timu hiyo na si Messi. Kwa Messi,  Barcelona sasa si mahali ambapo ataweza kucheza kwa ubora wake wa  zamani.

Mabadiliko kitakuwa kitu muhimu sana kwa staa huyo mshindi mara  nne wa tuzo ya Ballon d’Or. Lakini, Barca watabaki naye kisa jina na umaarufu wake.