Vigogo Ulaya macho yote kwa Andrey Santos
Muktasari:
- Msimu huu amecheza mechi 37 za michuano yote, amefunga bao moja na kutoa asisti nne, akitumika kama kiungo mkabaji na wakati mwingine kama kiungo wa kati.
MANCHESTER United inatarajiwa kukutana na upinzani mkali kutoka timu za Ligi Kuu England katika harakati zao za kumsajili kiungo wa Chelsea, Andrey Santos mwenye umri wa miaka 21.
Inaelezwa West Ham United na Juventus pia zimeonyesha nia ya kumtaka kiungo huyo ambaye kijana.
Mbali ya vigogo hao, tovuti ya Calciomercato ya Italia imeripoti kwamba Inter Milan pia inamfuatiliakwa karibu Santos na inaweza kutuma ofa dirisha lijalo.
Licha ya kwamba amekuwa hana nafasi ya kudumu kikosi cha kwanza, mara kadhaa ambazo amekuwa akipewa nafasi ya kucheza, Santos amekuwa akionyesha kiwango bora.
Mkataba wake wa sasa unamalizika mwaka 2030 na Chelsea haionekani kuwa na pingamizi la kukataa kumuuza ikiwa ofa nono itawasilishwa mezani.
Msimu huu amecheza mechi 37 za michuano yote, amefunga bao moja na kutoa asisti nne, akitumika kama kiungo mkabaji na wakati mwingine kama kiungo wa kati.
Myles Lewis-Skelly
TAARIFA za ndani zinadai Manchester United inaandaa mpango wa usajili wa kushtukiza wa beki wa kushoto wa Arsenal, Myles Lewis-Skelly, 19.
Inaelezwa tayari kuna mazungumzo ya awali kwa ajili ya dili hilo na upande wa mchezaji hauonekani kuwa na pingamizi lolote, hivyo kazi iliyobakia ni kuishawishi Arsenal.
Lewis-Skelly ni miogoni mwa wachezaji wanaoonekana ni kesho ya Arsenal, ikiwa ataondoka inaweza kuwa pigo kubwa kwa washika mitutu.
Bernardo Silva
KIUNGO wa Manchester City, Bernardo Silva, 31, anadaiwa kufikiria kukubali ofa ya kuhamia Barcelona mwisho wa msimu huu mara baada ya mkataba wake kumalizika.
Hata hivyo, inaelezwa, Silva anasita kutokana na ushindani wa nafasi ndani ya kikosi hicho ambacho idadi kubwa ya viungo wengi vijana. Mbali ya Barcelona, Silva pia yupo kwenye rada za vigogo kadhaa wa Saudi Arabia ambao wapo tayari kumpa mshahara mnono ili ajiunge nao.
Bruno Guimaraes
MANCHESTER United tayari imeanza mazungumzo na wawakilishi wa kiungo wa Newcastle United, Bruno Guimaraes, 28, ili kumsajili dirisha lijalo la majira ya kiangazi.
Man United inataka kusajili kiungo ili kuziba pengo la Casemiro, 34, anayetarajiwa kuondoka mwisho wa msimu. Licha ya kuonyesha nia ya kumsajili, taarifa zinadai Newcastle haina mpango wa kumuuza staa huyo tegemeo kwa sasa.
Robert Lewandowski
MSHAMBULIAJI mkongwe wa kimataifa wa Poland, Robert Lewandowski, 37, yupo katika kipindi cha kufikiria na kufanya tathmini kuhusu mustakabali wake msimu ujao.
Lewandowski ambaye kwa sasa anakipiga Barcelona anaangalia ikiwa atasaini mkataba mpya wa mwaka mmoja au ataondoka kutafuta changamoto mpya. Inaelezwa moja ya chaguo analolifikiria ni kujiunga na moja ya timu katika Ligi Kuu Marekani.
Leon Goretzka
AC Milan imeonyesha nia ya kumsajili kiungo wa kimataifa wa Ujerumani, Leon Goretzka, 31, mara tu atakapomaliza mkataba wake na Bayern Munich mwishoni mwa msimu huu.
Milan na Arsenal pia zinahitaji kumsajili fundi huyu. Hadi sasa hakuna mazungumzo yoyote ya mkataba mpya yaliyofanywa kati ya wawakilishi wa Bayern na wakala wake na Goretzka mwenyewe ndio ameomba kuondoka kwani anahitaji changamoto mpya.
Zeki Celik
LIVERPOOL imepiga hatua kubwa katika mazungumzo ya kumsajili beki wa AS Roma, Zeki Celik mwenye umri wa miaka 29, ambaye wakala wake ameweka wazi kuwa mchezaji huyo anataka kutafuta changamoto mpya nje ya Italia kwa msimu ujao.
Inaelezwa kuwa Liverpool wanamwona Celik kama chaguo sahihi la kuongeza ushindani katika upande wa kulia wa safu yao ya ulinzi.
Hugo Bueno
NEWCASTLE United inadaiwa kufanya makubaliano binafsi ya kumsajili beki wa Wolves, Hugo Bueno, 23, dirisha lijalo la majira ya kiangazi.
Bueno, ambaye ni raia wa Hispania, amekuwa akionyesha kiwango bora akiwa na Wolves licha ya timu hiyo kutofanya vizuri Ligi Kuu England msimu huu.
Inaelezwa Newcastle sasa inataka kuingia makubaliano na Wolves baada ya kumalizana na upande wa Bueno.