Msisitizo wa bodi kwa wachezaji, viongozi kuhusu kanuni
Muktasari:
- Miongoni mwa waliozungumza katika semina hiyo ni mkufunzi wa waamuzi Leslie Liunda aliyewashauri viongozi wa klabu ambao wako tayari kumpa mwaliko wa kwenda kuwapa elimu wachezaji ili wafahamu baadhi ya mabadiliko ya sheria.
WACHEZAJI na viongozi wa timu za mpira wa miguu Tanzania, wameshauriwa kuzipitia sheria za soka na maboresho yake ili kuzielewa vizuri katika msimu huu wa 2026-2027.
Hivi karibuni, Bodi ya Ligi ya Tanzania (TPLB) ilifanya semina na Wanahabari Tanzania kukumbushana vitu muhimu vya kuzingatia kwa msimu wa 2026-2027, ikiwemo maboresho ya sheria za mpira wa miguu.
Miongoni mwa waliozungumza katika semina hiyo ni mkufunzi wa waamuzi Leslie Liunda aliyewashauri viongozi wa klabu ambao wako tayari kumpa mwaliko wa kwenda kuwapa elimu wachezaji ili wafahamu baadhi ya mabadiliko ya sheria.
“Tunawategemea waandishi muwe na uelewa sahihi ili mnapoona matukio uwanjani yatafsiriwe kwa usahihi na taarifa zinapopelekwa kwa jamii ziwe ni zile zenye usahihi zitakazosaidia kujenga na kukuza mpira wa miguu nchini” alisema Liunda.
Alizifafanua sheria mbalimbali ambazo alisisitiza ni muhimu wachezaji wakazijua ili watakapokutana nazo uwanjani wasione ni kitu kigeni pale waamuzi watakapofanya uamuzi.
Baadhi ya sheria hizo ni Sheria 3:5 kifungu kidogo cha 8 9 10 (Law 3: The Players) inazungumzia mchezaji anayefanyiwa mabadiliko lazima atoke nje ya uwanja kwa wakati, ikiwa atachelewesha muda kupita kiasi asizidishe sekunde 10.
Endapo akizidi sekunde 10, adhabu yake ni mchezaji wa akiba anaweza kuingia uwanjani atakaporuhusiwa na mwamuzi baada ya dakika moja kupita tangu mchezo uanze tena.
Jambo ambalo Liunda alisisitiza kwamba: “FIFA ilifanya hivyo ili kupunguza makusudi ya baadhi ya wachezaji kujichelewesha hiyo inakuwa ni hasara kwa timu yake mfano, imetokea ni dakika za mwishoni mwa mchezo anaweza akaigharimu timu kwa kucheza pungufu, dakika moja uwanjani ni kubwa.”
Sheria nyingine ni ya 12.3 ya mpira wa kona (Law 12: Corner Kick) inayozungumzia mwamuzi ndiye atakayeamua kipa akianza kuudhibiti mpira anatakiwa kukaa nao si zaidi ya sekunde nane, akihesabiwa kwa ishara ya vidole na refa hadi ya muda huo, mpira itapewa timu pinzani.
“Sheria hiyo imetumika sana katika Kombe la Dunia 2026 kama mlifuatilia mechi vizuri, kuna makipa ili kuepuka adhabu hiyo wakawa wanajikuta wanapiga mipira bila utaratibu, sheria hiyo pia itatumika hadi katika mpira kona, nitoe wito kwa viongozi wa timu wanaohitaji msaada nipo tayari kuwaelekeza wachezaji, lakini ambao hawataki watakwenda kujifunzia uwanjani.” alisema Liunda.
Pia kuna sheria inayohusiana na vifaa (Sheria 4:1) inayozungumzia mchezaji hatoruhusiwa kutumia au kuvaa kitu chochote cha hatari isipokuwa vifaa vya ziada kama mapambo ilimradi visiwe na madhara.
Mbali na hilo, msimu huu wa 2026-2027, kuna kanuni ya matumizi ya teknolojia ya Video Support System (VS), ikilenga kupunguza utata katika uamuzi wa waamuzi wakati wa michezo.
Teknolojia hiyo hadi sasa imefanya matukio mengi kuamuliwa kwa haki ikiwemo kadi tatu nyekundu walizoonyeshwa Geofrey Manyasi wa Coastal Union, David Kameta ‘Duchu’ na Ibraheem Jabaar wote wa Simba.
WALICHOSEMA WACHEZAJI
Mshambuliaji wa Geita Gold iliyopanda Ligi Kuu Bara msimu huu, Yusufu Mhilu, alisema: “Wachezaji wengi hatuna kawaida ya kusoma sheria licha ya kuwa zipo mtandaoni ingawa makocha wanakuwa wanatuambia kuna maboresho ya sheria na kanuni hivyo tunapaswa kuwa makini ili tusizigharimu timu.”
Mchezaji mwingine aliyechangia hilo ni mshambuliaji mpya wa Polisi Tanzania, Daruwesh Saliboko aliyesema: “Kuna umuhimu kama wachezaji tujizoeshe kusoma sheria ingawa mara nyingi tunakuwa tunaelekezwa na makocha inapotokea maboresho.”
Kwa upande wa golikipa wa Dodoma Jiji, Ally Salim, alisema: “Mara nyingi tunaelekezwa na makocha na viongozi kabla ya kuanza msimu mwingine hivyo tunakuwa tumepata uelewa wa kujua kipi hakitakiwi kufanyika.”
Mbali na wachezaji, Katibu wa Dodoma Jiji, Fourtnatus Johnson, alisema: “Dodoma Jiji tuna utaratibu na tamaduni zetu kama ilivyo kwa kawaida kwa timu nyingine tunafanya semina na wachezaji ya kuwatambulisha wachezaji wapya desturi zetu kujua mazingira, mishahara inapotokea changamoto wanapaswa kufanya nini,” alisema kigogo huyo na kuongeza.
“Tunawafundisha kuhusu nidhamu dhidi ya wenyewe kwa wenyewe, makocha, viongozi, wanahabari na jamii kwa ujumla, ukiachana na hilo tunawakumbusha kuhusu sheria, tuna kawaida wiki moja kabla ya kuanza kwa ligi tunawaalika waamuzi kuja kuwafundisha pia inakuwa fursa kwa viongozi ambao hawakupata muda wa kuzipitia.”
VIONGOZI WA BODI
Mwenyekiti wa TPLB, Nassor Idrissa ‘Father’ alisema: “Wapenzi wa soka nchini niwaambie mpira wa miguu ni wa kila mtu, kuna maendeleo makubwa tulipotoka hadi tulipo kwa sasa, hivyo ni wajibu wa kila mtu kuhakikisha tunaleta maendeleo ya pamoja.”
Mtendaji Mkuu wa TPLB, Cornel Barnabas, naye alisema: “Nitoe wito kwa wanahabari muwe mstari wa mbele kuandika taarifa zenye uelewa sahihi wa kila eneo ili jamii iweze kupata usahihi wa mambo jambo litakalosaidia kukuza mpira wa miguu nchini.”