Huyu hapa Panenka mwenye panenka yake
Muktasari:
- Mbinu hiyo iliasisiwa na mchezaji wa Czechoslovakia, Antonin Panenka alipofunga penalti ya ushindi katika mikwaju ya penalti iliyoiwezesha Czechoslovakia kutwaa ubingwa wa Euro 1976 mjini Belgrade.
BELGRADE, SERBIA: KATIKA soka, Panenka ni mbinu ya kupiga penalti na mpigaji badala ya kuupiga mpira kwenda kushoto au kulia mwa kipa, huugusa kwa ustadi kutoka chini na kuuinua taratibu katikati ya lango.
Mbinu hiyo humdanganya kipa ambaye mara nyingi huwa tayari amejirusha upande mmoja wa lango, hivyo mpira hushuka polepole katikati na kuingia wavuni.
Mbinu hiyo iliasisiwa na mchezaji wa Czechoslovakia, Antonin Panenka alipofunga penalti ya ushindi katika mikwaju ya penalti iliyoiwezesha Czechoslovakia kutwaa ubingwa wa Euro 1976 mjini Belgrade.
Penalti hiyo ilimshinda kipa wa Ujerumani Magharibi, Sepp Maier, na kuipa Czechoslovakia taji la Ulaya.
Baada ya tukio hilo, mbinu hiyo ilijulikana duniani kote kwa jina la Panenka, huku mchezaji huyo akipata sifa na umaarufu mkubwa.
Hata hivyo, pia ilionekana kuwa mbinu yenye hatari kubwa kwa sababu ni ngumu kuitekeleza kwa usahihi. Endapo kipa atasoma nia ya mpigaji na kubaki katikati ya lango badala ya kujirusha, huwa rahisi kuudaka mpira.
Kutokana na hatari hiyo, penalti za aina ya Panenka hupigwa mara chache katika mechi za mtoano za kiwango cha juu. Baadhi ya waandishi wa habari za michezo wanadai kuwa kwa kawaida ni wachezaji wakubwa na wenye kujiamini ambao wanaweza kubeba lawama endapo watakosa, ndio hujaribu kutumia mbinu hiyo katika mashindano makubwa.
Awali, nchini Czech, mbinu hiyo iliitwa Vrsovicky dloubak (yaani “chip ya Vrsovice”), ikiwa ni kumbukumbu ya wilaya ya Vrsovice mjini Prague, ambako klabu ya Panenka, Bohemians, ilikojikita. Katika nchi nyingine, penalti hiyo inajulikana kwa majina tofauti. Nchini Italia huitwa Il cucchiaio (kijiko), Brazil huitwa cavadinha (uchimbaji mdogo), huku Argentina na baadhi ya nchi nyingine za Amerika Kusini ikiitwa penal picado, yaani penalti ya kuinua mpira taratibu.
Lakini, kuna simulizi yake na ni wazi kwamba kwa Panenka mwenyewe anajivunia kubuni pigo hilo la adhabu hata baada ya miaka 50 kupita.
“Penalti hiyo ilibadili maisha yangu,” anase,a Panenka anayejivunia miaka 50 tangu mkwaju wake wa kihistoria
Mbunifu huyo wa penalti maarufu anasema ujanja wake dhidi ya kipa Sepp Maier mjini Belgrade umeingia kwenye historia ya soka.
“Hasara pekee ni kwamba sipati mrabaha wowote,” anasema mchezaji huyo katika mahojiano maalumu akizungumzia miaka 50 sasa tangu alipokuja na maajabu ambayo yameendelea kuacha gumzo katika ulimwengu wa soka.
Katika mahojiano hayo Panenka anacheka kwa sauti nzito kana kwamba kumbukumbu zake bado zimejaa utundu, akiwa ameketi kwenye ofisi za Klabu ya Bohemians mjini Prague.
Akisimulia simulizi ya penalti yake hiyo ya kipekee na ya mapinduzi ambayo hayakuiwezesha tu Czechoslovakia kutwaa ubingwa wa Ulaya 1976 kwa kuifunga Ujerumani Magharibi, bali pia iliharibu uhusiano wake na kipa aliyemdhalilisha kwa mkwaju huo, Sepp Maier.
“Kwa miaka 35 (Maier) hakuwahi kusema neno hata moja kwangu,” anasema Panenka huku akitabasamu akidai ‘uhasama’ uligeuka na kuwa mkubwa zaidi.
“Nilisoma makala zilizoandika kwamba (Maier) alikuwa ameweka picha yangu kwenye ubao wa kulenga vishale (darts) ndani ya gereji yake na alikuwa akiitumia kufanya mazoezi. Hata hivyo, siku hizi tunaelewana vizuri.”
Juni 20, 2026 ilitimia miaka 50 tangu tukio hilo litokee katika Uwanja wa Red Star mjini Belgrade na kuingia kwenye historia ya soka duniani.
Baada ya dakika 120 kumalizika kwa sare ya mabao 2-2, Czechoslovakia na mabingwa watetezi wa dunia, Ujerumani Magharibi, walijikuta wakiikabili hali ambayo haikuwahi kutokea awali. Ilikuwa mara ya kwanza mshindi wa mashindano makubwa ya kimataifa kuamuliwa kwa mikwaju ya penalti.
Karibu isifike hatua hiyo kabisa. Mpango wa awali ulikuwa mchezo urudiwe, lakini ombi kutoka Shirikisho la Soka la Ujerumani (DFB) liliwashawishi waandaaji kutumia mikwaju ya penalti badala yake. Panenka anaamini uamuzi huo uliathiriwa na ukweli kwamba wachezaji wa Ujerumani tayari walikuwa wamepanga kwenda likizo zao.
Baada ya nyota wa Bayern Munich, Uli Hoeness, kukosa penalti ya nne ya Ujerumani kwa kupiga mpira juu ya lango, jukwaa lilikuwa tayari kwa Panenka aliyekuwa anakwenda kupiga penalti yake. Alisogea mbele akiwa na nafasi ya kuipa Czechoslovakia ubingwa, kisha historia ikaandikwa.
Alianza kwa kukimbia kwa kasi kuelekea mpira ulipokuwa kisha akapunguza mwendo sekunde ya mwisho na kuugusa kwa ustadi mkubwa. Mpira ukapaa taratibu katikati ya lango wakati Maier akiwa tayari amejirusha pembeni. Kwa sekunde chache mpira ulionekana kana kwamba umesimama hewani kabla haujatua wavuni. Ndipo penalti ya Panenka ikazaliwa.
Katika miongo iliyofuata, wachezaji wengi wamejaribu mbinu hiyo na kufanikiwa. Zinedine Zidane aliipiga kwa ustadi kwenye fainali ya Kombe la Dunia 2006, mpira ukigonga mwamba wa juu na kuingia wavuni. Andrea Pirlo naye alimwaibisha Joe Hart katika Euro 2012 kwa penalti ya aina hiyo.
Lakini siyo kila mchezaji amefanikiwa. Mwaka 1992, Gary Lineker, aliyekuwa akihitaji bao moja tu kufikia rekodi ya mabao 49 ya Bobby Charlton akiwa na England, alikosa penalti yake dhidi ya Brazil katika Uwanja wa Wembley na hivi karibuni zaidi, Brahim Diaz wa Morocco alipiga penalti ya aina hiyo kwenye fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika (Afcon 2025), lakini kipa wa Senegal, Edouard Mendy, aliidaka kirahisi.
Panenka huzitazama penalti hizo zote kwa fahari na furaha. “Ni furaha kubwa kuona wachezaji hawa wakitumia penalti yangu,” anasema.
“Hasara pekee ni kwamba sipati mrabaha wowote.”
Anasema kuna wakati aliwahi hata kufikiria kwamba kila mchezaji anayepiga penalti ya aina hiyo anapaswa kumlipa kiasi cha fedha kutokana na ubunifu aliouanzisha. “Wakati wa utawala wa Kikomunisti nchini Czechoslovakia nilizungumza na marafiki waliokuwa wakifanya kazi katika ofisi ya usajili wa hatimiliki. Nikitaka nisajili mbinu hiyo, lakini waliniambia haiwezekani. Ilikuwa jambo la kusikitisha,” anasema Panenka
Penalti yake hiyo kwenye fainali ya Euro 1976 haikuwa mara ya kwanza kuitumia, kwani miaka miwili kabla ya fainali za Belgrade, Panenka, aliyekuwa kiungo mbunifu wa Bohemians 1905 alianza mashindano ya kirafiki ya kupigana penalti na kipa wa klabu hiyo, Zdenek Hruska.
Kila siku baada ya mazoezi walibaki uwanjani kupiga penalti. Kwa kuwa alikuwa mshindani bora, Panenka alipendekeza wawekeane dau na kipa huyo, kwamba ikiwa angefunga penalti zote tano, Hruska angemnunulia bia au chokoleti. Lakini kama kipa angeokoa hata penalti moja, Panenka ndiye angelipa.
Mwanzoni Panenka alikuwa akipoteza dau mara kwa mara na kutumia fedha nyingi kumlipa kipa huyo, na ndipo akapata wazo lililobadili historia.
“Nilianza kufikiria makipa wengi huruka kuelekea upande mmoja au mwingine wa lango. Nikasema kwa nini nisiinue tu mpira katikati? Na ilifanya kazi mara moja,” anakumbuka Panenka, na kuanzia hapo alianza kushinda madau yote waliyowekeana na Hruska.
“Nilianza kushinda kila wakati, hivyo nikawa napata bia na chokoleti zote. Lakini matokeo yake nikaanza kunenepa,” anasema
Ingawa aliwahi kutumia penalti hiyo katika mechi za kirafiki na ligi ya ndani, haikuwa imejulikana nje ya Czechoslovakia hadi walipokwenda kwenye Euro 1976 nchini Yugoslavia. Huko ndiko kulikompa ujasiri wa kuitumia kwenye jukwaa kubwa zaidi.
“Nilijua tangu mwanzo kwamba ningepiga kwa namna hiyo kwa sababu hakuna aliyewahi kufanya hivyo na hakuna ambaye angeamini ningejaribu kwenye fainali,” anasema mkongwe huyo.
“Lakini sikuwa na uhakika wa asilimia 100 kwamba ningefunga. Nilikuwa na uhakika wa asilimia 1,000.”
Kwa Panenka, penalti hiyo siyo njia tu ya kufunga bao, kwani anasema ubunifu wa kuibuni ulihitaji ujasiri wa kipekee, lakini pia mazoezi makubwa ili kuimudu ipasavyo. “Huwezi kuwa na kimoja bila kingine,” anasema.
Ukitazama video ya penalti yake leo, utaona tofauti kubwa na nyingi zinazopigwa siku hizi maana hakukuwa na kukimbia kwa mbwembwe wala kumtazama kipa kwa muda mrefu, ambapo alikimbia moja kwa moja kwa kasi, akamshawishi Maier kuamini kwamba angepiga kwa nguvu.
Sekunde ya mwisho akapunguza mwendo na kuuinua mpira taratibu katikati ya lango, huku Maier akiwa tayari amejirusha kushoto.
Kwa Panenka, huo ni uzuri wa kipekee.
Anasema: “Nimewahi kusikia ikiitwa penalti ya ‘jani linaloanguka’ na napenda jina hilo. Inafanyika kwa uzuri sana.”
Baada ya kushinda ubingwa wa Euro 1976, Panenka na wenzake walirejea nyumbani wakitarajia mapokezi makubwa, lakini hali ilikuwa tofauti.
“Tulitarajia sherehe au angalau kutambuliwa, lakini hakukuwa na chochote kikubwa. Tulisema, ‘sisi ni mabingwa wa Ulaya! Wakatujibu, ‘sasa iweje? Ligi inaanza tena kesho, rudini kazini.’,” anasema.
Lakini aliporejea Bohemians, penalti hiyo iligeuka kuwa silaha aliyotumia kwa nadra, ambapo anakadiria alipiga penalti nyingine 15 katika maisha yake ya soka, lakini alitumia mtindo wa panenka mara tatu tu. Miongoni mwa mechi maarufu ni ushindi dhidi ya Ufaransa katika kufuzu Euro mjini Bratislava 1979.
Na katika hali ya kushangaza anasema ni mara moja tu alishindwa kufunga. “Ilikuwa kwenye mechi ya kirafiki dhidi ya klabu ndogo kusini mwa Bohemia. Kulikuwa na mvua kubwa sana na kipa alikuwa amesimama kwenye dimbwi la maji. Nafikiri hakutaka hata kujirusha. Alisimama tu na kuudaka mpira,” anakumbuka mchezaji huyo.
Leo hii, akiwa na umri wa miaka 77, Panenka na penalti yake wanajulikana duniani kote akiwa anaamini wazazi wamekuwa wakirithisha kizazi hadi kizazi jina hilo kupitia YouTube na mitandao ya kijamii. Hata hivyo, umaarufu wake bado humshangaza.
“Hivi karibuni nilikuwa ndani ya ndege Madrid ikisubiri kuruka. Mtu mmoja akanitambua. Ghafla ikatokea foleni ndefu ya watu waliotaka kupiga selfie na mimi kiasi kwamba hata safari yetu ilichelewa,” anasema
Ni wachezaji wachache sana katika historia ambao majina yao yamegeuka kuwa sehemu ya msamiati wa soka kutokana na ubunifu wao kama ilivyo kwa Cruyff Turn, ndivyo ilivyo pia kwa Panenka ambaye mbinu yake ya upigaji penalti imeendelea kuwa alama ya ujasiri, ubunifu na ustadi.
Panenka anasema kama angepiga penalti ya kawaida siku ya fainali dhidi ya Ujerumani huenda Czechoslovakia isingeshinda ubingwa wa Ulaya na isingebadili maisha yake, wala isingeliandika jina lake katika historia ya soka. Lakini, miaka 50 baadaye kinachokumbukwa siyo medali yake wala kombe pekee ni uamuzi wake wa sekunde chache uliogeuza mambo na kumfanya mchezaji wa kawaida kuwa sehemu ya simulizi isiyofutika katika mchezo huo.
“Penalti niliyopiga kweli ilibadili maisha yangu. Na ukweli kwamba bado niko hapa miaka 50 baadaye nikizungumzia tukio hilo ni jambo la ajabu kabisa. Nina furaha sana kwamba niliipiga,” anasema.