Prime
Mitaa haitamsahau kwa urahisi Francis Mponjoli Kifukwe
MITAA haitamsahau Francis Mponjoli Kifukwe. Umauti ulimkuta nchini India alikokuwa anaugua. Tukapata nafasi ya kumuaga katika Ukumbi wa Karimjee. Akazikwa kwao Kyela juzi Jumamosi. Mungu amrehemu.
Hakukuwa na watu wengi katika ukumbi wa Karimjee. Sababu ni rahisi tu. Kwa mujibu wa sensa yetu inadaiwa watu zaidi ya asilimia 80 nchini wamezaliwa baada ya Mwalimu Julius Nyerere kufariki dunia mwaka 1999.
Kwa mujibu wa sensa yetu pia nadhani watu asilimia 70 inawezekana wamezaliwa baada ya Francis Kifukwe kupambana kuisaidia Yanga akiwa kama mfadhili. Vijana wengi kuanzia mashabiki hadi viongozi wa mpira wa sasa, pia waandishi wa habari hawakuuona na kuufaidi utawala wa Kifukwe Yanga. Walikuwa wadogo.
Mfano ni waandishi wa habari. Wengi hawakuhudhuria msiba wa Kifukwe kwa sababu hawamfahamu. Wengi wanaamkia katika nyumba ya Dotto Magari na hawakuupa msiba wa Kifukwe umuhimu mkubwa.
Lakini Francis Kifukwe alikuwa roho ya Yanga. Mzungu wa roho. Alikuwa na pesa ingawa hakuwa milionea. Namna alivyoibeba Yanga katika mambo mengi akiwa mhandisi tu iliwashangaza wengi. Na inatukumbusha mpira wetu ulikotoka.
Wakati huo matajiri wanavizia kuwasajili wachezaji usiku wa manane. Wanawatorosha wachezaji kutoka nyumbani kwao au katika hoteli ambayo mtani amempangia mchezaji. Wakati huo umafia ukiwa juu. Kifukwe ndio alikuwa silaha kubwa ya Yanga. Sio kwamba alikuwa anakwenda mwenyewe, hapana, pesa yake ilikuwa inatumika kufanikisha jambo.
Mchezaji wa zamani wa Yanga, Aaron Nyanda alininong’oneza, Kifukwe alikuwa mtu safi kiasi kwamba wakati anamsajili alimuahidi kuendelea kumsomesha kwa pesa yake ya mfukoni hadi atakapomaliza elimu yake yote ya dunia.
Wakati huo kukiwa hakuna mdhamini wa ligi wala mdhamini wa klabu watu kama kina Kifukwe ndio walikuwa waokozi. Sawa, wachezaji walikuwa hawasafiri kwa ndege kwa kudeka kama ilivyo leo. Wakati huo Simba na Yanga zinakwenda kilomita 850 kufika Mbeya kwa usafiri wa basi. Maisha yalikuwa ya kimaskini tofauti na leo, hata hiyo pesa ya basi ilikuwa shughuli kuipata. Kifukwe ndio alikuwa ‘sterling’ wa Yanga.
Kifukwe alitawala Yanga baada ya kuondoka kwa Watanzania wenye asili ya Asia kina Abbas Gulamali. Haikuwa kazi rahisi sana na vijana wengi wa kileo maarufu kama Gen Z wangepata shida kuzipenda timu hizi kwa mazingira ya wakati ule.
Ilikuwa ni kitu cha kawaida tu kwa wakubwa wetu wa Kariakoo kusikia wameacha madeni katika nyumba za kulala wageni maarufu kama Guest House. Hawa kina Kifukwe ndio walikuwa waokozi wa nyakati hizo.
Chanzo kikubwa cha mapato kilikuwa ni kiingilio cha getini. Yaani kiingilio hiki hiki ndio kiendeshe timu, pia kilipe wachezaji mishahara na bonasi zao. Hakukuwa na chanzo kingine cha mapato zaidi ya kutegemea pesa za kina Kifukwe.
Leo maisha yamekuwa matamu. Wadhamini wapo kedekede. Kuanzia katika ligi yenyewe na katika klabu. Lakini hata ambao wanaonyesha mpira wetu ‘live’ Azam TV nao wametia pesa katika timu.
Wafadhili wa hizi timu pia ni mabilionea. Kina Ghalib Said Mohamed. Matokeo yake wakubwa wanadeka siku hizi. Timu inasafiri kwa ndege kwenda Dodoma wakati zamani isingeweza kufikirika. Ni Mwanza tu ndipo timu ingeweza kusafiri kwa ndege.
Maisha kabla ya haya yalikuwa magumu na tuliwahitaji watu kama kina Kifukwe. Jaribu tu kufikiria, kama timu ilikuwa inapata shida kusafiri kwa ndege kwenda Dodoma ilikuaje katika mechi za kimataifa na timu ilipaswa kusafiri kwenda Misri kucheza mechi za kimataifa? Walisimama kina Kifukwe kuficha aibu.
Mitaa haiwezi kumsahau Francis Kifukwe. Kitu cha kushangaza katika yote haya ni hakuwa mtu wa kupenda sifa. Alikuwa mkimya na hakupenda kuongea na waandishi wa habari. Alikuwa hapatikani kiurahisi.
Sisi ambao tulimhitaji zaidi tulikutana naye katika baa iliyoitwa Bakulutu pale Kinondoni ambayo alikuwa anakunywa kilaji na washkaji zake. Yanga iliendeshwa pale zaidi. Maamuzi mazito ya Yanga na furaha ya Wanayanga ilikuwa inafanyika pale.
Wakati watu wengi wenye msaada mkubwa katika timu wanapenda kuabudiwa na hawataki mtu mwingine apate sifa zaidi yao, Kifukwe hakuwa mtu wa namna hii. Ndiye mtu ambaye aliwatafutia Yanga mfadhili anayeitwa Yusuf Manji. Kama angekuwa mbinafsi na anayependa kuabudiwa zaidi asingewatafutia Yanga Manji.
Lakini Ijumaa wakati Yanga wakimuaga Kifukwe pale Karimjee rais wao wa sasa, Injinia Hersi Said alikiri Kifukwe ndiye aliyemsaidia kufanikisha kupata baadhi ya nyaraka muhimu za mali za Yanga alizozifahamu wakati wa utawala wake.
Mtu mwingine mwenye roho mbaya na ambaye hapendi maendeleo yapatikane nje yake asingeweza kufanikisha hili kwa urahisi. Hersi anakiri simu yake ya kwanza kwa Kifukwe ilifanikisha kila kitu.
Pia Kifukwe pia ndiye aliyekuwa anasisitiza zaidi wazo la Yanga kuwa kampuni. Watu wabinafsi ambao wameishika klabu huwa hawapendi kufanikisha michakato hii kwa sababu michakato hii ikileta maendeleo basi umuhimu wao klabuni unaondoka. Kifukwe hakuwa mtu wa namna hii.
Mungu amlaze mahala pema peponi. Mitaa haitamsahau Francis Kifukwe. Alikuwa mtu mwema, pia ni vizuri kuwakumbusha Gen Z, walikuwepo watu kama kina Kifukwe wakati timu hizi zikiishi maisha magumu.
Kitu wanachokiona kwa sasa kutoka kwa kina Ghalib wasidhani kama kilikuwepo zama hizo. Walilazimika kuwepo watu kama Francis kwa ajili ya kuivusha timu kutoka katika kizazi kimoja kwenda kingine. Apumzike kwa amani Francis Mponjoli Kifukwe.