Mohamed Muya aachiwa msala KMC
Muktasari:
- Muya amejiunga na KMC FC kwa mkataba wa mwaka mmoja baada ya kutokuwa na timu yoyote tangu mara ya mwisho alipoachana na Coastal Union, Aprili 8, 2026, kufuatia kudumu kwa siku 184, tangu alipojiunga na kikosi hicho rasmi, Oktoba 6, 2025.
UONGOZI wa KMC FC, umefikia makubaliano ya kumwajiri aliyekuwa Kocha Mkuu wa Fountain Gate, Geita Gold na Coastal Union, Mohamed Muya ili kukiongoza kikosi hicho cha Kinondoni, Dar es Salaam msimu wa 2026-2027, katika Ligi ya Championship.
Muya amejiunga na KMC FC kwa mkataba wa mwaka mmoja baada ya kutokuwa na timu yoyote tangu mara ya mwisho alipoachana na Coastal Union, Aprili 8, 2026, kufuatia kudumu kwa siku 184, tangu alipojiunga na kikosi hicho rasmi, Oktoba 6, 2025.
Akizungumza na Mwanaspoti, Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa KMC FC (CEO), Daniel Madenyeka alikiri kufikia makubaliano hayo na Muya wakiamini uzoefu wake ni chachu ya kukirejesha kikosi hicho katika Ligi Kuu baada ya kushuka msimu wa 2025-2026.
“Ni kweli tumefikia makubaliano hayo ya kumwajiri Muya kukiongoza kikosi chetu kwa msimu wa 2026-2027, tumempa mkataba wa mwaka mmoja tukiamini atairudisha tena timu yetu Ligi Kuu kutokana na uzoefu wake aliokuwa nao,” amesema Madenyeka.
Aidha, Madenyeka amesema aliyekuwa pia kaimu kocha mkuu wa timu hiyo, Imani Mwalupetelo aliyekiongoza kikosi hicho hadi hatua ya kushuka daraja ataendelea kubakia kikosini humo, japo atakuwa ni kocha msaidizi wa Muya kwa msimu wa 2026-2027.
KMC iliyoshuka daraja baada ya kumaliza mkiani mwa nafasi ya 16, katika Ligi Kuu Bara kwa msimu wa 2025-2026 na pointi tisa, ilianza msimu na Kocha Mkuu, Mbrazil Marcio Maximo ki-sha kuondoka Desemba 6, 2025, kutokana na matokeo mabaya.
Baada ya kuondoka kwa Maximo uongozi wa timu hiyo ukamtangaza aliyekuwa Kocha wa Zimamoto ya visiwani Zanzibar, Abdallah Mohamed ‘Baresi’ Desemba 30, 2025, huku akiwa na uzoefu wa kuzifundisha maafande wa JKT Tanzania na Tanzania Prisons.
Baresi aliyeifundisha pia Mlandege ya visiwani Zanzibar, alidumu KMC FC kwa siku 94, baada ya kuondoka Aprili 3, 2026, kutokana na matokeo mabaya na nafasi yake kukaimiwa na Imani Mwalupetelo aliyeiongoza hadi mwisho wa msimu wa 2025-2026.