Kisa 'mishepu', Hamisa, Poshy Queen wacharuka
Muktasari:
- Kwa hapa Tanzania, kinadada wengi wanafanya hivyo ikiwamo watu maarufu na wanaoonekana kuposti picha zao wamekuwa wakisemwa tofauti kutokana na mionekano yao.
ISHU ya kuongeza miili hasa shepu kwa wanawake siyo jambo geni. Wasanii wengi wa kike duniani wamekuwa wakikimbilia kufanya upasuaji 'surgery' kuongeza au kupunguza shepu zao au sehemu nyingine ya mwili zikiwamo, pua, mashavu na nyinginezo.
Kwa hapa Tanzania, kinadada wengi wanafanya hivyo ikiwamo watu maarufu na wanaoonekana kuposti picha zao wamekuwa wakisemwa tofauti kutokana na mionekano yao.
Wapo wanaodhani wametumia dawa za kichina za kuongeza shepu, wengine wanadhani wamefanya upasuaji na hili limekuwa likiwakera wahusika.
Hata hivyo, wapo wanaokiri wazi kutumia dawa hizo kwa madai wanatamani kuwa na shepu kubwa, lakini wapo ambao mionekano yao ya umbo ni ya kurithi na hawataki kabisa kusikia mambo ya kufanya upasuaji na kufeki maumbo yao.
Mwanaspoti liliongea na baadhi yao ambao wanadai wamekuwa wakikumbana na changamoto hiyo ya kuambiwa wamefeki maumbo yao na kudai wanachukizwa na maneno hayo.
Hamisa Mobetto
"Tena bora niseme hili. Huwa nachukizwa sana kila nikiposti picha Instagram watu wanakimbilia kukomenti eti nimefanya 'surgery' ili kuongeza ukubwa wa makalio yangu. Naumia sana kuambiwa hivyo, huwa najiuliza kwani kila mwenye makalio makubwa ni lazima aonekane amefanya 'surgery'? Au wapi niliwahi kutangaza nimefanya 'surgery' ya umbo?"
"Halafu wanaosema hivyo hawaeleweki wanaeleza nini, hawajitambui wanachokisema, kipindi cha nyuma walikuwa wanaosema natumia dawa za Kichina kusema ukweli nimechoshwa na maneno hayo, nimeamua kusema hili," alisema Hamisa na kuongeza kinachomsabaisha kuwa na shepu hiyo ni matunzo mazuri anayopata kwa mume wake Aziz KI .
"Ieleweke ni matunzo kwa mume wangu Aziz KI, pia familia yangu imenilea vizuri kwa kula chakula bora tangu nikiwa mdogo, sijawahi kuijua 'surgery' wala dawa za kichina," alisema.
Careen Simba
Ni msanii wa Bongo Movie aliyepata umaarufu baada ya kuhusishwa kimapenzi na nyota wa Yanga, Pacome Zouzoua. Hata hivyo, alikanusha madai yao licha ya ukaribu waliokuwa nao tangu nyota huyo atue Jangwani miaka miwili iliyopita.
Kuhusu mwonekano wake, Careen alisema amekuwa akiandamwa sana na madai ya kufanya 'surgery' ili kuongeza shepu lake, jambo ambalo amekuwa akilipuuza.
"Mara zote nimekuwa nikipuuza maneno ya mitandaoni ya mimi nimetengeneza shepu. Hadi kufikia kupuuza, nimechukizwa kwani mtu hata historia yako haijui anakurupuka tu na kuamza kuandika shepu ya kutengeneza. Sasa ngoja niwaambie, hii shepu ni kutoka katika familia yangu, siyo 'surgery', watu mitandaoni hatujuani vizuri jamani nakerekwa sana mimi na wanavyoniingiza kwenye listi ya waliofanya 'surgery'."
Poshy Queen
Alijipatia umaarufu mitandaoni baada ya kuwa na uhusiano na msanii wa Bongo Flover Harmonize. Kutokana na umbo lake, amekuwa akipata wakatiu mgumu kila anapoposti picha zake Instagram na wengi wanasema kafanya 'surgery'. Msikie mwenyewe:
"Mimi sijawahi bwana kufanya 'surgery' yoyote. Hayo ni maneno tu watu wanasema na mwishowe unachukia na kuamua kuwaitikia tu na kuwaacha na kuamini kile wanachokiamini wao. Ukweli ukiniangalia mimi na mama yangu tumefanana sana maumbo yetu, hivyo ni vya kurithi hivi."
Wema Sepetu
Staa huyu wa Bongo Movie aliwahi kuandamwa sana anatumia dawa za Kichina, kisha akaambiwa amefanya 'surgery' ya kutengeneza shepu na ndiyo maana akawa na mkalio makubwa. Kutokana na maneno hayo, mama yake, Miriam Sepetu aliamua kuvunja ukimya na kueleza wanaomsema mwanaye anatumia dawa za Kichina wakome maana kalio lake ni orijino na amelirithi kutoka kwake.
Wapo mastaa waliokumbwa na skendo kama hizo akiwamo Kajala Masanja, Irene Uwoya, Wellu Sango, Shamsa Ford na wengine wengi.