Kipigo cha Kagera Sugar chamuachia maumivu Kaseja
Baadhi ya wachezaji wa
Muktasari:
- Kagera Sugar na Geita, zote zimepanda Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu, baada ya awali kushuka daraja.
Kocha Mkuu wa Kagera Sugar, Juma Kaseja amesema ameumizwa na kipigo cha mabao 6-2, ilichokipata timu yake dhidi ya Geita Gold, lakini akaahidi kurejea mazoezini kutafuta tiba ya upungufu wa kikosi chake.
Kagera Sugar ilikutana na kipigo hicho cha mabao 6-2, katika wa Ligi Kuu Tanzania Bara, uliochezwa jana Jumamosi, Agosti 22, 2026 usiku kwenye Uwanja wa Bukombe, Geita.
Hicho ni kipigo kikubwa zaidi kwa timu moja kufungwa tangu kuanza kwa msimu huu wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Katika mchezo huo, mabao ya Geita yalifungwa na Richardson Ngondya katika dakika za 12 na 63, Obrey Chirwa (dk 24,69) na Yusufu Mhilu (dk38, dk45), wakati mabao ya Kagera Sugar yalifungwa katika dakika ya 41 na Hassan Mwaterema na Robert Mkandya katika dakika za majeruhi.
Akizungumzia matokeo hayo, Kaseja amesema yamemsikitisha lakini analazimika kukubaliana nayo na kuelekeza nguvu katika mchezo unaofuata.
"Matokeo haya yanaumiza. Ukiangalia sio kwamba tumecheza vibaya sana isipokuwa tumefanya makosa mengi ambayo wapinzani wetu wameyatumia kutuadhibu.
"Tunarudi uwanja wa mazoezi kuangalia wapi tuliteleza na kurekebisha ili mchezo ujao tuweze kupata matokeo chanya," amesema Kaseja ambaye ni kipa wa zamani wa Simba na Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars).
Kagera Sugar itacheza mchezo wake unaofuata dhidi ya Mashujaa, Alhamisi wiki ijayo kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma.
Nayo Geita baada ya ushindi huo, itaumana na Azam FC katika mchezo utakaopigwa Ijumaa ijayo kwenye Uwanja wa Bukombe.
Kagera Sugar na Geita, zote zimepanda Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu, baada ya awali kushuka daraja.