Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Okello agusia bato lake na Chama


KULE Simba kuna moto unaowashwa na kiungo wao Clatous Chama ambao mashabiki wa timu zingine hawaufurahii lakini Yanga nako kuna mtu mwingine ana balaa, huyu ni Allan Okello, vilevile wengine wanachukia kiwango chake. Sasa raia huyo wa Uganda ameamua kufunguka kuhusu Chama.


Chama tangu amerejea Simba kuanzia dirisha dogo la Januari 2026, namba zake zimeanza kushtua akifunga jumla ya mabao manane kati ya hayo, sita ameyafunga akiwa na Wekundu hao wa Msimbazi wakati mawili aliyafunga alipokuwa Singida Black Stars.

Kiungo huyo pia amefanikiwa kutengeneza asisti sita ambazo zote amezipika akiwa hapo Simba na kumfanya kuhusika kwenye jumla ya mabao 14, lakini moto wake zaidi ni kwamba amebeba tuzo tano za mchezaji bora wa mechi katika michezo mitano mfululizo.

Okello naye ana balaa lake, akianzia dirisha dogo la Januari 2026 kama ilivyo kwa Chama, akifanikiwa kufunga mabao tisa akimfikia Prince Dube anayecheza naye pale Yanga ambaye yeye ameanza mwanzo wa msimu.

Kiungo huyo ukiacha kufunga, amefanikiwa kutengeneza asisti saba mpaka sasa na kumfanya kuhusika kwenye jumla ya mabao 16 ndani ya Ligi Kuu Bara akiwa kwenye kiwango bora zaidi hatua ambayo ikaanzisha mijadala juu ya viwango vya viungo hao wawili wa kigeni ambao wote wametua Januari 2026.

Akizungumza na Mwanaspoti kwenye mahojiano maalum, Okello alisema alikuwa anamjua Chama muda mrefu hata kabla ya kuja nchini kujiunga na Yanga akisema kiungo huyo Mzambia ni mchezaji mwenye ubora mkubwa.

Okello alisema hana shida kwa mashabiki wakibishana juu ya nani bora kati yake na Chama na kwamba mjadala huo unampa nguvu ya kuendelea kujituma zaidi kuipigania Yanga katika kufikia malengo yake.

“Namfahamu Chama ni mchezaji mkubwa amekuwa kwenye kiwango kizuri kwa nyakati tofauti, nasikia na kuona hiyo mijadala kutoka sehemu tofauti, naichukulia kwenye mlengo chanya, sina shida, inanipa faraja kwamba kuna kitu kizuri tofauti nakifanya hapa,”  alisema Okello ambaye alisajiliwa Yanga akitokea Vipers ya Uganda.

“Mimi sina mtu ambaye nakimbizana naye, ninachofanya ni kuhakikisha timu yangu inafanikiwa, nataka kuhakikisha kwamba Yanga inakuwa bingwa ndio maana nitapambana kuona timu tunashinda mechi zetu, sina tatizo na Chama, namtakia kile la kheri akiwa na timu yake.”

Aidha Okello alisema hana presha yoyote katika kukimbizana katika kufunga kati yake na Chama. Kwake kitu pekee anachokitanguliza ni Yanga kushinda mechi zake.

“Presha pekee niliyonayo ni kutamani Yanga kushinda mechi zetu, kitu muhimu hapa ni timu kupata ushindi au pointi tatu, kama ambavyo nilisema Chama ni mchezaji mzuri lakini niseme hakuna mchezaji ambaye nashindana naye kwenye ligi wala ndani ya timu yetu.

“Unajua niwe wazi, huwezi kucheza kwa kiwango cha juu kila wakati, inawezekana nikaja kushuka au inawezekana hata Chama akaja kushuka, hiyo ni kawaida na hiyo ndio soka, nikisema niichukue presha ya kushindana na mtu itanishusha, kitu muhimu kwangu kama sitafunga au kutoa asisti basi Yanga ishinde.”

Wawili hao wanakutana na ushindani mkali kutoka kwa kiungo wa Azam, Feisal Salum mwenye mabao 12 na asisti 8 hadi katika Ligi Kuu.