Singida BS yatuma salamu, ikiichapa Mogadishu
Muktasari:
- Mogadishu City ndiyo ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 10 kupitia Naby Bangoura, aliyeitumia vizuri nafasi aliyoipata na kuwapa Wasomalia hao matumaini ya kupata ushindi wao wa kwanza kufuatia kutoa suluhu katika mchezo wao wa kwanza dhidi ya Simba.
BINGWA mtetezi wa Kombe la CECAFA Kagame, Singida Black Stars imefufua matumaini ya kutetea taji hilo baada ya kuibuka na ushindi mnono wa mabao 4-1 dhidi ya Mogadishu City katika mchezo wa Kundi B uliopigwa leo, Jumanne kwenye Uwanja wa Kigali Pele, Rwanda.
Baada ya kuanza vibaya michuano hiyo kwa kuchapwa mabao 2-0 na Jamus SC katika mchezo wa kwanza, Singida Black Stars iliingia uwanjani ikihitaji ushindi ili kuendelea kubaki kwenye mbio za kutinga hatua ya nusu fainali.
Mogadishu City ndiyo ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 10 kupitia Naby Bangoura, aliyeitumia vizuri nafasi aliyoipata na kuwapa Wasomalia hao matumaini ya kupata ushindi wao wa kwanza kufuatia kutoa suluhu katika mchezo wao wa kwanza dhidi ya Simba.
Hata hivyo, Singida Black Stars haikukata tamaa dakika tatu baadaye, kiungo mpya Henry David aliisawazishia timu hiyo kabla ya Mathew Tegisi kuifungia bao la pili dakika ya 16 na kuigeuzia upepo wa mchezo Singida.
Kabla ya mapumziko, Henry alirejea tena kambani na kufunga bao lake la pili dakika ya 44, lililoifanya Singida kwenda mapumziko ikiwa mbele kwa mabao 3-1.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi kutoka kwa Singida na dakika ya 53, Tegisi naye akafunga bao lake la pili la mchezo na la nne kwa timu yake, akihitimisha ushindi muhimu wa mabao 4-1.
Ushindi huo umeonyesha nguvu ya usajili mpya wa Singida Black Stars, kwani mabao yote manne yalifungwa na wachezaji wapya. Henry, aliyesajiliwa akitokea Fountain Gate, alifunga mabao mawili huku Tegisi, aliyewasili kutoka Pamba Jiji, naye akifunga mawili na kuthibitisha thamani yao ndani ya kikosi hicho.
Matokeo hayo yanaifanya Singida Black Stars kufufua matumaini ya kutetea ubingwa wa CECAFA Kagame huku ikisubiri mchezo wake wa mwisho wa hatua ya makundi ambao utaamua hatma yake ya kutinga hatua ya nusu fainali dhidi ya Simba.
Katika mchezo wa mwisho wa hatua ya makundi, Singida BS itacheza dhidi ya Simba ambayo inashikilia rekodi ya timu iliyotwaa ubingwa wa michuano hiyo mara sita.