Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Kwa Diarra, tuendelee kuwaheshimu wazungu na kanuni zao?

JICHO Pict


KANUNI lazima ziheshimiwe. Wakati mwingine huwa zinakuwa za kijinga, lakini lazima ziheshimiwe. Wazungu huwa wanasema ‘rules must be obeyed’. Wakati mwingine hata kama kanuni ni za kijinga, lakini lazima ziheshimiwe.


Na katika watu huwa wanaheshimu kanuni zao basi ni wazungu. Labda ndio maana mwezi ujao ifikapo tarehe 27 Djigui Diarra atatimiza miaka 31 akiwa Tanzania. Hata miaka 30 ilimkuta hapa hapa Dar es Salaam akiwa na klabu yake ya Yanga.


Nadhani kilichomleta Dar es Salaam kutoka Bamako miaka kadhaa iliyopita kilikuwa kimo chake. Basi. Hakuna kingine. Wazungu wana kanuni zao na vigezo vyao. Kipa lazima awe mrefu. Mabeki wa kati lazima wawe warefu.

Wachezaji wa nafasi nyingine uwanjani sio lazima wawe warefu, lakini kipa lazima awe mrefu. Mshambuliaji wa kati anaweza kuwa mfupi kama ilivyo kwa Sergio Kun Aguero na wengineo wengi, lakini Aguero hawezi kukaa langoni hata kwa dawa. Naamini hiki ndicho kilichomleta Diarra Tanzania.

Kuna watu hawaamini vinginevyo. Ni hadithi ile ila ya Marcio Maximo alipokuja nchini kwa mara ya kwanza mwaka 2006. Aliamini katika urefu wa Ivo Mapunda kuliko uhodari wa Juma Kaseja. Tulipiga kelele kadri tulivyoweza, lakini Maximo akaziba masikio kwa sababu aliamini katika kanuni.

Kwa Diarra, wakati mastaa wenzake wa Mali wakiwa wanapanda ndege kurudi katika timu zao za Ulaya, yeye anapanda ndege kurudi Tanzania. Kipa wa ubora wake kutoka Afrika Magharibi kama angekuwa mrefu nadhani na yeye mida hii angekuwa anapanda ndege kurudi Ulaya.

JICH 01

Wakati Yves Bissouma anarudi England kuendelea kukipiga na Tottenham Hotspur, Amadou Haidara anaenda zake Ufaransa kuendelea na majukumu yake na klabu ya Lens, El Bilal Toure anaelekea zake Uturuki kuendelea na majukumu yake na Besiktas, Diarra anaweza kuliwahi pambano la fainali keshokutwa dhidi ya Azam akiwa na jezi ya Yanga.

Hapo hapo inastaajabisha unapoitazama timu hii ya taifa ya Mali. Hawa kina Bissouma wanatamba zao Ulaya, lakini wanapokuja katika timu ya taifa wanalazimika kutii amri za Diarra pale uwanjani na wanajikuta katika mikono salama licha ya kwamba kipa wao anacheza Afrika Mashariki.

Sio wao tu, hata wakazi wa Mali pamoja na mastaa kibao wa zamani wa Mali tuliowaheshimu kina Mamadou Diarra, Sadio Kanoute, Seydou Keita na wengineo wanalazimika kuheshimu ukweli kwamba lango lao linalindwa na kipa ambaye anaishi na kufanya mazoezi kule Kigamboni.

JICH 02

Diarra ana kila kitu ambacho makipa wengi wa Ulaya hawana. Yuko vizuri juu na chini. Katika michuano hii ya Afcon amethibitisha hivyo kule Morocco. Kinachosikitisha ni ukweli kwamba amebanwa na kanuni za Wazungu kwamba kipa lazima awe mrefu.

Taifa la Mali linaangaliwa kwa makini na wazungu ambao wanazurura katika miji mbalimbali ya nchi hiyo kama ambavyo wanazurura nchi nyingi za Afrika Magharibi kama vile Senegal, Togo, Nigeria, Cameroon na nyingine wakiamini kuna vipaji vingi.

Siamini kama hawakumuona Diarra akiwa katika lango la Stade Mallen pale Bamako. Tatizo ni hizo kanuni ambazo wamejiwekea. Sisi Afrika wakati mwingine tunazipuuza, lakini wao huwa hawafanyi hivyo. Ndio maana Diarra akaangukia kwetu.

JICH 03

Na ukitaka kujua kwamba sisi tunazipuuza kanuni hizi na tunaweka mbele kipaji kuliko mambo mengine ni ukweli kwamba hata pale katika lango la Mali, Diarra anamuweka benchi kipa, Ismael Diawarra mwenye urefu wa futi 6’4 ambaye amezaliwa Sweden.

Ingekuwa kwa wazungu Diawarra angecheza mbele ya Diarra, lakini kwetu sisi kipaji kwanza. Labda ndio maana sitashangaa pia kwamba baada ya michuano hii wazungu bado hawatamtaka Diarra, lakini kuna klabu za Afrika, hasa zile za Afrika Kusini zinaweza kumtaka Diarra.

Wale rafiki zetu wa Afrika Magharibi kina Misri, Algeria, Morocco na Tunisia wamejiwekea kanuni kwamba hawataki makipa wa kigeni katika ligi zao, lakini ni wazi kwamba wanammezea mate Diarra. Shida inaweza kuja kutoka katika timu za Afrika Kusini ambazo zina uwezo mkubwa wa kipesa.

JICH 04

Kitu kingine ambacho tunapaswa kusifu katika hili la Diarra ni jicho la Injinia Hersi Said. Wengi huwa tunajiuliza ‘Hersi alimtoa wapi Diarra?’

Ilikuwa ni rahisi kuwapata kina Aziz Ki, Pacome Zouzoua, Maxi Nzingeli na wengineo kwa sababu mataifa ya Ivory Coast na Congo tumeyaweka mkononi kwa sasa. Lakini kwenda kumpata kipa kama Diarra kutoka Mali nadhani jicho lake lilitulia.

Naamini pia baada ya miaka kadhaa, Hersi atatazama nyuma na kugundua kwamba uhamisho wa Diarra kutoka Stade Mallien kuja Yanga huenda ukawa ndio uhamisho wake bora zaidi aliowahi kuufanya akiwa kama Rais wa Yanga. Pengine zaidi ya uhamisho wa kina Pacome na Fiston Mayele.

JICH 05

Inatufundisha kutuliza kichwa katika masuala ya uhamisho wa wachezaji. Labda kuna makipa mahiri wapo Togo, lakini hatujui. Wachezaji wazuri bado wamo humu humu ndani Afrika, lakini kwa sababu tumejawa na uvivu wa kusaka vipaji ndio maana kila siku tunawagombania wachezaji hawa hawa walio ndani ya ligi yetu.

Lakini inatufundisha kukubali ukweli kwamba kwa siku hizi kina Hersi na wenzao wamejitahidi kutuletea wachezaji wenye ubora ambao wanakubalika katika timu za taifa za mataifa makubwa.

Kuanzia kwa wachezaji wa ndani hadi makipa kama Diarra na Moussa Camara wa Simba nadhani tumepiga hatua fulani ya kuachana na wachezaji magarasa wa kigeni ambao walitawala katika soka letu miaka kadhaa nyuma.