Tanzanite Queens kuangukia hapa Kombe la Dunia
Muktasari:
- Tanzanite ni miongoni mwa timu nne kutoka Afrika zilizofuzu michuano hiyo ambayo kwa mwaka huu itapigwa Poland kuanzia Septemba 5 hadi 27, 2026.
DROO ya hatua ya makundi ya Kombe la Dunia Wanawake chini ya miaka 20, itachezeshwa leo Ijumaa saa 10 jioni jijini Lodz, Poland, huku Timu ya Taifa ya Tanzania ya Wanawake chini ya umri huo, Tanzanite Queens ikisubiri kufahamu wapinzani wake.
Tanzanite ni miongoni mwa timu nne kutoka Afrika zilizofuzu michuano hiyo ambayo kwa mwaka huu itapigwa Poland kuanzia Septemba 5 hadi 27, 2026.
Mashindano hayo yanashirikisha timu 24, Afrika ukiitoa Tanzanite Queens, zingine zilizofuzu ni Nigeria, Ghana na Benin.
Tanzanite imepangwa katika chungu cha nne pamoja na Italia, Ureno, Ecuador, Benin na New Caledonia, hiyo ikimaanisha itapangwa na timu moja kutoka kila chungu kilichobaki.
Chungu cha kwanza zimo Japan, Hispania, Brazil, Ufaransa, Korea Kaskazini na wenyeji Poland, huku chungu cha pili kikijumuisha Marekani, Nigeria, Colombia, Mexico, Korea Kusini na England. Chungu cha tatu kinaundwa na Ghana, Canada, New Zealand, Argentina, China na Costa Rica.
Kutokana na upangaji huo, Tanzanite inaweza kudondokea kwenye kundi gumu lenye timu kama Hispania, Marekani na Canada, au Japan, England na Argentina na zote zina rekodi nzuri katika soka la wanawake vijana.
Hata hivyo, droo inaweza pia kuipa Tanzanite kundi la ushindani wa wastani zaidi likijumuisha Poland ambao ndio mara yao ya kwanza kushiriki mashindano hayo, Mexico na Costa Rica, jambo ambalo linaweza kuongeza matumaini ya kufanya vizuri hatua ya makundi.
Hii ni mara ya kwanza Tanzanite kucheza Kombe la Dunia kwa umri huo na katika timu hizo Tanzania, Benin na Poland pekee ndio timu changa.
Kwa Afrika, Tanzanite na Benin ndio wageni kwenye michuano ya umri huo kwani Ghana inakwenda kushiriki mara ya nane baada ya mwaka 2010, 2012, 2014, 2016, 2018, 2022, 2024, huku Nigeria ikifuzu mara 12 (2002, 2004, 2006, 2008, 2010, 2012, 2014, 2016, 2018, 2022, 2024 na sasa 2026).
Safari ya Tanzanite ilianzia raundi ya pili baada ya kuitoa Angola kwa jumla la mabao 7-0, ikishinda mabao 4-0 mechi ya kwanza na marudiano 3-0.
Raundi ya tatu ikaitoa Kenya kwa penalti 3-1 baada na mechi mbili zilimalizika kwa sare ya bao 1-1 na raundi ya nne ikakutana na Cameroon na ilipoteza mabao 3-1 kule Cameroon na marudiano kushinda mabao 2-0 kwenye Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar na kuifanya Tanzanite Queens kufuzu Kombe la Dunia kwa faida ya bao la ugenini kufuatia matokeo ya jumla kuwa 3-3.