Gor Mahia, Vipers mechi ya kisasi
Muktasari:
- Gor Mahia ilifanya balaa katika mchezo wake wa kwanza wa michuano hiyo baada ya kuichapa APR mabao 5-0 huku Vipers nayo ikiingia katika mchezo huu ikiwa na morali baada ya kuanza kwa ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya CF GR/SIAF ya Djibouti.
BAADA ya kuanza kwa kishindo mashindano ya CECAFA Kagame Cup kwa kuichapa APR ya Rwanda mabao 5-0, Gor Mahia ya Kenya leo Jumatatu inarejea tena uwanjani ikiwa na kibarua kingine kigumu dhidi ya Vipers ya Uganda katika mchezo wa kundi A.
Gor Mahia ilifanya balaa katika mchezo wake wa kwanza wa michuano hiyo baada ya kuichapa APR mabao 5-0 huku Vipers nayo ikiingia katika mchezo huu ikiwa na morali baada ya kuanza kwa ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya CF GR/SIAF ya Djibouti.
Mchezo huu unatarajiwa kuwa wa ushindani mkubwa kutokana na historia ya timu hizi katika mashindano ya CECAFA Kagame Cup.
Hii itakuwa mara ya pili kwa Gor Mahia na Vipers kukutana katika michuano hiyo, baada ya kukutana mwaka 2018 ambapo Wakenya waliibuka na ushindi wa mabao 2-1 katika hatua ya robo fainali.
Katika mchezo huo wa mwaka 2018, Vipers ndiyo ilianza kupata bao kupitia Taddeo Lwanga ambaye baadae alitua Simba, lakini Gor Mahia ilisawazisha kupitia Jacques Tuyisenge kabla ya Francis Mustafa kufunga bao la ushindi na kuipeleka timu yake hatua ya nusu fainali.
Kwa upande wa historia ya Gor Mahia katika CECAFA Kagame Cup, ni moja ya klabu zenye mafanikio makubwa kwenye ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, ikiwa imewahi kutwaa ubingwa wa mashindano hayo mara tatu, mwaka 1980, 1981 na 1985.
Vipers nayo imekuwa moja ya timu zinazoheshimika Uganda katika miaka ya karibuni, ikiwa na uzoefu mkubwa wa mashindano ya kimataifa na sasa inataka kutumia nafasi hii kulipa kisasi dhidi ya Gor Mahia baada ya kupoteza mchezo wao wa mwisho.
Mechi nyingine ambayo inatarajiwa kuchezwa leo ni kati ya CF GR/SIAF dhidi ya APR ya hapa Rwanda.