Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Maajabu ya Arsenal ikitinga fainali UEFA 2026

ARSENAL Pict

Muktasari:

  • Wimbo huo ambao ndio unaotumiwa na Arsenal kama wimbo wao wa klabu, unaimbwa sana leo kufuatia timu hiyo kufuzu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya ikiiondosha Atletico Madrid kwa jumla ya mabao 2-1.

MITAA ya Jiji la London leo wimbo mmoja tu unapigwa, nao si mwingine bali ni ule uliotungwa na kuimbwa na mwanamuziki Muingereza, Louis Mark Dunford uliopewa jina la The Angel lakini unafahamika zaidi kama North London Forever.

Wimbo huo ambao ndio unaotumiwa na Arsenal kama wimbo wao wa klabu, unaimbwa sana leo kufuatia timu hiyo kufuzu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya ikiiondosha Atletico Madrid kwa jumla ya mabao 2-1.

Ushindi wa bao 1-0 lililofungwa na Bukayo Saka, nahodha wa mechi hii ya nusu fainali ya mkondo wa pili iliyochezwa Mei 5, 2026 kwenye Uwanja wa Emirates jijini London nchini England, limetosha kuipeleka Arsenal pale Budapest nchini Hungary kucheza fainali ya michuano hiyo itakayochezwa Mei 30, 2026. Inaisubiri Bayern Munich au PSG zinazorudiana Jumatano hii Mei 6, 2026 baada ya mechi ya kwanza PSG nyumbani kushinda 5-4 dhidi ya Bayern.

ARS 01

Bao la Saka dakika ya 45 lililotokana na shuti la Leandro Trossard kuokolewa na Jan Oblak kisha mpira kumkuta mfungaji aliyemalizia kiurahisi, limeipeleka Arsenal fainali ya michuano hiyo kwa mara ya pili, ikiwa imepita takribani miaka 20 tangu mara ya mwisho kufuzu 2006 na kupoteza mbele ya Barcelona kwa mabao 2-1.

Maajabu ya fainali hii ni kwamba, ukiweka kando Arsenal kuwa imefuzu bila ya kupoteza mechi kati ya 14 ilizocheza za michuano hiyo msimu huu zaidi ya kutoka sare mbili pekee ikishinda 12 ikiambulia clean sheet tisa, kuna ishu inawahusu vijana watatu waliokuwepo kikosini wakati klabu hiyo ikiweka rekodi.

Ipo hivi; Yaani wakati Arsenal inacheza fainali ya UEFA mwaka 2006 pale Paris nchini Ufaransa, kuna nyota wawili ndani ya kikosi hicho ambao wamekuwa sehemu ya waliofuzu fainali ya mwaka huu walikuwa hawajazaliwa, huku mwingine akiwa na miezi mitatu pekee tangu azaliwe.

Kipa namba tatu aliyekuwa benchi na Kepa Arrizabalaga wakimshuhudia David Raya akiondoka na clean sheet ya tisa UEFA msimu huu, Tommy Setford aliyezaliwa Machi 13, 2006 akiwa sasa ana miaka 20, ndiye alikuwa na miezi mitatu tangu azaliwe mara ya mwisho Arsenal inacheza fainali ya michuano hii.

Lakini Myles Lewis-Skelly aliyezaliwa Septemba 26, 2006 akiwa amebakisha miezi minne kufikisha miaka 20 mwaka huu, alikuwa hayupo duniani kipindi hicho Arsenal inacheza fainali ya UEFA.

Pia Max Dowman aliyezaliwa Desemba 31, 2009 akienda kutimiza miaka 17 miezi saba ijayo, yeye ilibidi isubiriwe miaka mitatu mbele kuja kuzaliwa tangu mara ya mwisho Arsenal kucheza fainali UEFA, lakini mwaka huu, alikuwa benchi kushuhudia chama lake likipata mafanikio hayo.

ARS 02

Baada ya kujitoa kwa hali ya juu na kupambana mwanzo mwisho, hatimaye Arsenal sasa imefika kileleni kukaribia mafanikio yao.

Katika msimu ambao umejaa wasiwasi na taabu kwao, unaweza kusema unakaribia kumalizika kwa furaha na mafanikio makubwa mara mbili.

Uliweza kuona mara tu baada ya filimbi ya mwisho jinsi ushindi huu ulivyokuwa na maana kubwa, wachezaji wakipiga makofi kwa furaha, ndani yake wana nafasi ya kushinda kila kilicho muhimu msimu huu navyo ni taji la Ligi Kuu England na Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Hata kufika tu fainali ya Ligi ya Mabingwa ikiwa ni mara ya pili pekee katika historia yao na ya kwanza tangu 2006, tayari ni mafanikio makubwa kwa Arsenal. Wachache walitarajia hili kutokea wakati Mikel Arteta alipochukua usukani, kutokana na hali mbaya ya timu ilivyokuwa Desemba 2019, na hata misimu michache iliyofuata, lakini wengi wao walimkatia tamaa mapema. 

Hata hivyo, Arteta ameirejesha heshima ya klabu na kuirudisha katika hadhi ya juu na sasa inasubiri kumalizia hatua chache ikitakiwa kushinda mechi zote nne zilizobaki ndani ya siku 24 kutoka sasa ili kufikia malengo hayo.

Hili ndilo waliloliota. Budapest sasa inatoa fursa kwa kocha huyo mzaliwa wa San Sebastián nchini Hispania miaka 44 iliyopita, kuwa wa kwanza kuiletea Arsenal ubingwa wa Ligi ya Mabingwa. Na furaha hii inaweza kufanya nini kwa mbio zao za ubingwa wa ligi? Cha kushangaza, huu ulikuwa usiku wa kusahau hilo. Ilikuwa ni kuhusu kilichotokea hapa.

Ushindi huu wa nusu fainali dhidi ya Atletico Madrid bao 1-0 na kufanya matokeo ya jumla kuwa 2-1 kufuatia sare ya 1-1 wiki iliyopita nchini Hispania, ulikuwa mfano halisi wa msimu wao mzima. 

Arsenal walipaswa kupambana. Ilikuwa mechi yenye presha kubwa, huku uongozi wa bap ukiwa mwembamba sana.

Hata hivyo walivumilia. Waliendelea kusonga mbele licha ya kuwa na presha kubwa.

Walikuwa na bahati pia, hasa kwenye uamuzi wa matukio mawili ya penalti, lakini Arteta angeweza kusema walistahili hiyo bahati kwamba ilikuwa ni bahati ile ile inayorudi baada ya muda.

Wachezaji muhimu walioibeba timu hiyo walikuwa ni wale waliokumbana na changamoto mbalimbali msimu huu. Bukayo Saka aliyekuwa nje kwa muda mrefu kutokana na majeraha hadi mashambulizi ya Arsenal yakapoteza makali, ndiye aliyefunga bao muhimu. Viktor Gyokeres, ambaye mara nyingi amekosolewa kama usajili butu, ndiye aliyeanzisha shambulizi la bao hilo. Myles Lewis-Skelly, kijana aliyekuwa akipotezewa mara kwa mara hadi kuibuka mjadala wa kuuzwa kwake, alileta nguvu waliyoikosa kwa muda mrefu. Na walihitaji sana nguvu hiyo dhidi ya timu inayopambana kama Atletico.

ARS 03

Gyokeres alitoa mchango huo, licha ya kukosolewa mara nyingi kwa kushindwa kulinda mpira, hapa alikuwa akipambana nao, akiwaweka mabeki wa Atletico kwenye wakati mgumu. Kwa kifupi alikuwa kero kwao.

Bao la Arsenal lilitokana na juhudi hiyo. Gyokeres alifuatilia mpira uliokuwa unaonekana kupotea, akafanikiwa kupenya upande wa kulia na kufungua nafasi kubwa eneo la hatari.

Changamoto ilikuwa nafasi hiyo kuwa karibu na mstari wa mwisho, hivyo kupunguza chaguo zake. Hata hivyo alifanya uamuzi sahihi kwa kuinua mpira kwenda kwa Leandro Trossard, ambaye shuti lake liliokolewa vizuri na Jan Oblak.

Lakini Saka tayari alikuwa ameshafanya harakati zake. Tangu arejee, amesifiwa kwa uwezo wake wa kukata kutoka kulia, na inashangaza Atletico hawakuliona hilo. Hivyo akajikuta katikati ya mabeki wawili na kufunga kirahisi. Gyokeres alipaswa kufanya hivyo pia baadaye, lakini hakuweza.

Inaonekana msimu wa 2025-26 wa Gyokeres hauwezi kukamilika bila kasoro kidogo. Alipaswa kufunga bao la pili dakika ya 65, baada ya pasi nzuri kutoka kwa Piero Hincapie.

Badala yake, akiwa peke yake akitazamana na kipa, alikosea na kupiga mpira juu ya lango.

Ilisemwa awali kwamba tofauti na mechi ya PSG dhidi ya Bayern Munich, hii ingekuwa nusu fainali ya mapambano ya karibu sana. Na kweli ilikuwa hivyo.

Kulikuwa na tukio ambalo Antoine Griezmann na Robin Le Normand walishangilia kwa nguvu kupatiwa goal kick badala ya kona.

Ilikuwa wazi kabisa hii ingekuwa mechi ya aina hiyo, ambapo maamuzi mengi yalitegemea tafsiri ya mguso.

Arsenal pia waliweza kulalamika, baada ya Trossard kuonekana kusukumwa na Griezmann eneo la hatari. Hata hivyo, tukio hilo lilionekana halikuwa na uzito kama madai ya Atletico.

Kubwa zaidi lilikuwa pale Giuliano Simeone alipokuwa karibu kufaidika na kosa la Declan Rice, lakini akazuiwa na Gabriel Magalhães. Iliamuliwa kuwa kona, lakini ilionekana ingeweza kuwa penalti.

Dakika chache baadaye, Griezmann alianguka baada ya kukanyagwa na Riccardo Calafiori, lakini mwamuzi akatoa faulo kwa Arsenal kutokana na kosa la Marc Pubill awali dhidi ya Gabriel Magalhães.

Simeone alikasirika sana. Arsenal walijibu kwa nguvu ile ile. Walishinda mapambano. Walishinda mechi. Na sasa wana nafasi ya kushinda kila kitu muhimu.

Yote kwa yote, wimbo wa The Angel maarufu North London Forever unaendelea kusikika pale London na viunga vyake, huku Afrika Mashariki wakiburudika na Finale, yake Bien na Alikiba.

Kula chuma hicho; North London forever,
Whatever the weather,
These streets are our own,
And my heart will leave you never,
My blood will forever,
Run through the stone.

Kwa upande mwingine, twende hapa; Leo silali, ni kukesha mitungi nawasha nachoma,
Tena sijali, yamewashinda yao yetu wataweza,
Leo silali, ni kukesha mitungi nawasha nachoma,
Tena sijali, yamewashinda yao yetu wataweza, ah-ah-ah-ah
Ah, watatii (finale)
Ah, watatupenda (finale)
Eh, referee (finale)
Puliza kipenga (finale)
Oh, watatii (finale)
Watatupenda (finale)
Referee (finale)
Puliza kipenga (finale)