Prime
Hili la kutotumia vyumba linahitaji uchunguzi
HABARI kwamba wachezaji wa Azam FC walipata athari za kitu ambacho hakijajulikana mara baada ya mechi yao na TRA United, zinaweza kuwa za kawaida, lakini hazifai kupuuzwa kutokana na hofu ya njama za timu kuwekewa madawa ya kulewesha kwenye vyumba vya kubadilishia nguo kuzidi na sasa kuingia kwenye mechi za ndani.
Tumezoea kuona timu za nje zikikataa kuingia kwenye vyumba hivyo wakati wa mechi za Ligi ya Mabingwa au Kombe la Shirikisho, lakini uzalendo hutufanya tusihoji kama kweli huwa kuna njama kama hizo.
Lakini kama hiyo hofu imeingia hadi kwa timu za ndani, tatizo lishaanza kuwa kubwa. Hii ni vita ya nje ya uwanja ambayo inapoteza imani katika soka kwamba mshindi hupatikana kwa makandokando na si kwa jitihada za uwanjani.
Ni wiki chache zimepita tangu Yanga wafanye uamuzi ambao si wa kawaida wa kutumia nyumba iliyo jirani na Uwanja wa Meja Jenerali Isamhuyo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kubadilishia nguo badala ya eneo walilotengewa ndani ya uwanja huo walipokwenda kucheza dhidi ya Simba.
Yanga hawajuti kwa kitendo chao na badala yake wanajisifu kuwa walitegua mtego waliowekewa ambao hawajawahi kuusema unahusu nini.
Yawezekana ni mambo ya kiimani kwamba wapinzani wao walifanya mambo ya kishirikina kwenye chumba hicho kama zilivyo hisia baina ya watani hao wa jadi. Hilo si tatizo kubwa kwa kuwa kisayansi halina athari zozote labda za kisaikolojia tu kwamba wachezaji waamini wenzao wana nguvu za ziada na hivyo kuona jitihada zao haziwezi kufua dafu mbele ya waliolindwa kishirikina.
Lakini kama hofu ni ya kuhisi chumba kimepuliziwa dawa zenye athari katika mwili zinazoweza kuwachosha wachezaji ndani ya muda fulani, basi tatizo ni kubwa na halina budi kuanza kufanyiwa kazi ili mpira wetu uchezwe katika mazingira ambayo ni sawa na yasiyo na hofu za aina yoyote.
Badala ya kuridhika kuzipiga faini timu zinazojaribu kuepuka mitego hiyo, ni muhimu mamlaka zianze kufanya uchunguzi wa hofu hizo ili kujua njia za kuimaliza.
Tunazijua timu kama za kutoka Misri, Algeria, Morocco, Afrika Kusini au Tunisia haziwezi kutishwa na madai kuwa wapinzani wao hapa Tanzania wameshughulikia vyumba vyao kishirikina. Huko walishavuka muda mrefu. Lakini timu kutoka nchi hizo na nyingine zinapogoma kutumia vyumba vya kubadilishia nguo, maana yake madai ni makubwa zaidi ya imani za kishirikina.
Hapo ndipo mamlaka za soka zinapotakiwa ziingilie katika kutafuta kiini cha hofu hizo na kutafuta suluhisho.
Habari kwamba wachezaji wa Azam FC walikuwa wakiendesha baada ya mechi yao na TRA United ndiyo inaweza kuwa mwanzo wa uchunguzi huo.
Kuna vitu vinaonekana vya kawaida, lakini vina madhara makubwa katika soka letu. Ikifikia muda mashabiki wakaanza kuamini kuwa washindi au bingwa hupatikana kwa mbinu za kutumia dawa za kudhoofisha wachezaji wa timu pinzani, maana yake matokeo ya uwanjani hayatakuwa na maana na itafikia muda watu watapotea viwanjani.
Katika mechi za karibuni, maeneo kadhaa viwanjani yanaonekana hayana watu, hata inapokuwa mechi muhimu na hali inaelekea hivyo katika mechi za watani wa jadi. Mambo ni mengi yanayoweza kusababisha mahudhurio viwanjani kupungua, yakiwemo maendeleo ya kielektroniki ambayo sasa yamewapelekea mashabiki mechi kwenye viganja vyao.
Lakini mambo hayo yakizidishwa na tuhuma au madai ya matumizi ya njama za ziada za nje ya uwanja, mahudhurio yatapungua zaidi. Na yakipungua, hata mechi zinazorushwa moja kwa moja zitapoteza mvuto kwa vile sehemu kubwa ya majukwaa itakuwa tupu.
Tuache kuzoea mambo yanayoonekana si ya kawaida bali tufanyie kazi kila taarifa inayoonekana kuathiri mchezo wetu unaopendwa na mamilioni ya Watanzania. Tuache kudhani kuwa adhabu kubwa na faini kubwa ndio suluhisho la kila tatizo.
Uchunguzi wa matukio yanayojirudiarudia ndio utaweza kutatua tatizo kabla ya kuwa sugu. Na pengine utamaduni huo unatengeneza ajira kwa watu wajinga katika klabu wanaoishi ama kwa kujidai wana mafundi wanaoweza kudhoofisha wachezaji wa timu pinzani kimazingara au wana kemikali zinazoweza kuathiri kiwango cha wachezaji wa timu pinzani.
Ni wakati sasa kwa mamlaka kuchukua hatua ili klabu zetu ziingie kwenye usasa badala ya kupoteza muda mwingi kukimbia mitego ambayo pengine haziijui na hazina ushahidi nayo.