Prime
Injinia Hersi alikuwa Rabat akimsikiliza Mwalimu au?
RAFIKI yangu, Injinia Hersi Said alikuwepo katika fainali ya juzi ya michuano ya ligi ya mabingwa wa Afrika kati ya Far Rabat dhidi ya Mamelodi Sundowns. Mechi ilichezwa Rabat mji ambao naambiwa Hersi ana ofisi zake katika cheo chake alichopewa na CAF kama bosi wa klabu Afrika.
Mamelodi imeibuka mabingwa baada ya pambano la juzi. Kule kwao Pretoria walishinda 1-0, halafu juzi pale Rabat wametoka sare ya 1-1 shukrani kwa kipa wao, Ronwen Williams ambaye alicheza penalti ya wenyeji kipindi cha pili. Hersi alipomtazama Williams akicheza penalti sidhani kama alisikia wivu kwa sababu na yeye ana kipa bora kikosini kama Williams. Djigui Diarra.
Hata hivyo, kuna kitu ambacho Hersi alipaswa kujifunza zaidi katika mechi hii. Timu yake Yanga walicheza na Mamelodi Sundowns Machi na April mwaka 2024. Mamelodi walikuwa timu ya kawaida tu uwanjani. Kuanzia Dar es salaam hadi Pretoria. Kulikuwa na sababu mbili. Sababu ya kwanza ni ubora wa Yanga yenyewe. Yanga walikuwa moto hasa wakati ule.
Pambano la marudiano Yanga waliwakosa Khalid Aucho na Pacome Zouzoua lakini bado walikuwa katika ubora wao pale Pretoria. VAR iliwadhulumu Yanga bao la Aziz Ki. Baadaye Clement Mzize akakosa bao la wazi ambalo lingeweza kuwazamisha Mamelodi na kuwapeleka Yanga katika nusu fainali yao ya kwanza ya michuano hii. Hadi leo Mamelodi huwa hawaamini waliponaje katika mechi ile.
Sababu ya pili ni Mamelodi wale nao hawakuwa kama hawa. Hawa wa juzi ambao wametwaa ubingwa wanaonekana wamebadilika . Nusu fainali walicheza dhidi ya Waarabu Esparance Du Tunis na fainali wamecheza dhidi ya Far Rabat. Walihama kutoka kwa mwarabu mmoja wakaenda kwa mwarabu mwingine. Walihama kutoka Tunisia wakaenda Morocco.
Mambo mawili yametokea tangu Yanga wadhulumiwe bao la Aziz Ki. Yanga wameshuka halafu Mamelodi wamepanda. Yanga ya leo ingekandwa vizuri tu na Mamelodi hii, lakini Yanga ile ya kina Aziz ingeweza kuwakanda vizuri tu hawa kina Far Rabat au Esparance Du Tunis. Ni hapa ndipo Hersi na genge lake wanaweza kushika kalamu na karatasi na kujifunza kitu.
Kuna namna wenzetu wanapambana kupata mwendelezo wa ubora. Wenzetu wanapambana kuendelea kuwa juu. Hii ni kazi ngumu ambayo inamkabili Hersi na wenzake pale Jangwani. Kuwa juu. Kuendelea kuwa juu. Kufanya mabadiliko ambayo yanaiweka timu kuwa pale pale ilipo. Namna ambavyo Mamelodi na Yanga wamepishana katika ubora kuanzia pale bao la Aziz lilipokataliwa mpaka leo ni jambo la kujifunza.
Kuna suala la kuweka hela kwa wachezaji wa maana. Kuna suala la uchunguzi kuhusu wachezaji wa maana. Kukaa juu kwa muda mrefu sio jambo la masikhara. Tangu ujio wa Pacome Zouzoua, Maxi Nzingeli na Aziz Ki, Yanga haijaleta tena wachezaji wa kariba ile. Haishangazi kuona mpaka leo kina Pacome hawajapata wapinzani katika nafasi zao. Nina mashaka na namna mambo yanavyokwenda katika uhamisho wa wachezaji pale Yanga.
Msimu uliopita waliletwa wachezaji wengi wapya kikosini lakini ni Mohamed Hussein Tshabalala ndiye ambaye amesimama na kuhesabiwa kama mchezaji aliyeweka mchango mkubwa klabuni. Dirisha la Januari Yanga walivamia Uganda na kumchukua Alain Okello ambaye walau ameweza kwenda sambamba na kina Pacome. Wengine wameshindwa. Mchezaji kama Lassine Kouma sijui anafanya nini Yanga.
Hersi na wenzake pia wanaweza kwenda Misri na kujifunza kitu kutoka kwa klabu kama Al Ahly. Huwa wanafanya nini katika kipindi kama hiki wakiwa na wakati mgumu? Kwa sasa wanatazamiwa kwenda kushiriki michuano ya Shirikisho. Katika michuano ya ligi ya mabingwa wa Afrika ambayo imemalizika juzi Al Ahly waliishia robo fainali. Huwa wanakubali kwamba wamekuwa na msimu ujao.
Hata hivyo, msimu ujao unaweza kuona wakitwaa ubingwa wa ndani Misri na wa Shirikisho. Msimu ule mwingine utashangaa wakirudi kwa nguvu tena katika michuano ya ligi ya mabingwa na kutwaa kombe lenyewe. Hawa wakubwa huwa wanaanguka kidogo kisha wanaibuka tena. Sisi tunaanguka kwa muda mrefu.
Timu kama Wydad Casablanca inaonekana kama vile imepotea. Huwa haipotei jumla. Sasa hivi wamechutama na kuingia chimbo kujipanga. Wakitoka huko wanaweza kwenda moja kwa moja katika fainali za ligi ya mabingwa wa Afrika na kutwaa kombe lenyewe. Hapa ndipo akina Hersi wanapopaswa kujifunza. Wenzetu huwa wanafanya nini kuendelea kusimika wachezaji wa maana katika kikosi na kutopotea kwa muda mrefu. Nadhani shida kubwa ni uwekezaji wa wachezaji mahiri katika kikosi.
Mchezaji kama Buba Jammeh alikujaje Yanga? Alikuja ghafla kwa maelekezo ya Kocha Pedro Concalves. Nadhani umefika wakati wa kuachana na tabia ya wazungu. Tabia ya kuamini zaidi maelekezo ya kocha katika masuala ya uhamisho. Makocha wengi huwa wanawachukua wachezaji wanaowafahamu kishkaji zaidi bila ya kujali sana mwelekeo wa timu.
Mchezaji kama Mohamed Damaro amefikaje Yanga. Kama huyu ndiye ambaye ametegemewa kuchukua nafasi ya Khalid Aucho basi lazima timu ishuke kutoka ilipokuwa. Hapa ni suala la maamuzi zaidi. Kuna wakati Yanga inachukua maamuzi ya kibabe zaidi dhidi ya nyota wake muhimu kwa ajili ya kuwatia adabu. Hata hivyo mbele ya safari inagundulika kwamba maamuzi hayakuwa sahihi.
Ni kama lilipokuja suala la Clatous Chotta Chama. Waliamua kumpotezea lakini muda umekuja kuhukumu kwamba hayakuwa maamuzi sahihi kwao kuachana na Chama. Walau Okello amekuja kufuta aibu lakini ukweli ni hayakuwa maamuzi sahihi sana kuachana na Clatous ambaye bado kichwa chake kinabeba maarifa mengi uwanjani.
Eneo jingine ambalo kina Hersi wanapaswa kulitazama ni eneo la benchi la ufundi. Baada ya kuondoka Manuel Gamondi Yanga haijawahi kuwa ile tena. Kuna shida mahala. Makocha ambao wameletwa baadaye wameshindwa kuirudisha timu katika uhai. Kocha kama Roman Folz hakuja na wasifu wowote mkubwa na alionekana kama vile ni kocha wa majaribio.
Yanga wanahitaji kufanya kama kile ambacho Simba wamefanya. Simba wamekwenda Afrika Kusini na kumchukua kocha mzoefu na mwenye sifa zake, Steve Barker. Sio tu kwamba ni mzoefu lakini hadi majuzi akiwa na Stellenbosch watu waliona namna alivyoibadili timu hiyo ndogo kuwa tishio pale Afrika Kusini. Yanga na Simba kwa walipofika hawahitaji tena kocha wa majaribio katika kutimiza ndoto zao.
Bahati nzuri kwa sasa wamepata muda mrefu wa kutafakari ni kocha gani ataweza kuwafaa msimu ujao. Huu sio muda wa kukurupuka. Kocha mpya atakuja na wachezaji wapya na Yanga inapaswa kurudi kusimama iwe ile ile ambayo watu wanaifahamu. Tabia ya kuendelea kuwategemea akina Pacome kila kukicha ni ishara kwamba kuna usajili mwingi wa wachezaji unafeli klabuni.