Lewandowski ataka pointi 100 Barcelona
Muktasari:
- Katika mchezo huo uliochezwa Pamplona, Barcelona ilishinda mabao 2-1, huku Lewandowski akifungua ukurasa wa mabao dakika ya 81 kabla ya Ferran Torres kuongeza la pili dakika ya 86. Bao la Raul Garcia dakika ya 88 halikutosha kuzuia ushindi huo.
PAMPLONA, HISPANIA: MSHAMBULIAJI wa FC Barcelona, Robert Lewandowski, amewapa changamoto wachezaji wenzake kuhakikisha wanafikia alama 100 katika msimamo wa La Liga baada ya ushindi muhimu dhidi ya CA Osasuna.
Licha ya Barcelona kuongoza ligi kwa tofauti ya pointi 14, mshambuliaji huyo mkongwe amesema haitoshi kushinda ubingwa pekee, bali wanapaswa kufikia mafanikio makubwa yaliyowahi kuwekwa na makocha Tito Vilanova na Jose Mourinho.
Katika mchezo huo uliochezwa Pamplona, Barcelona ilishinda mabao 2-1, huku Lewandowski akifungua ukurasa wa mabao dakika ya 81 kabla ya Ferran Torres kuongeza la pili dakika ya 86. Bao la Raul Garcia dakika ya 88 halikutosha kuzuia ushindi huo.
Akizungumza baada ya mechi, Lewandowski amesema: “Lengo letu ni kushinda kila mechi ili kufikia pointi 100. Hata kama tutashinda LaLiga mapema, bado tunapaswa kushinda mechi zilizobaki.”
Ameongeza: “Kushinda LaLiga ni jambo zuri sana. Sherehe zake ni za kipekee kwa mashabiki na jiji zima, lakini mpaka tushinde rasmi, ni bora tusizungumze sana.”
Mbali na hilo, nyota huyo alimpongeza Marcus Rashford kwa mchango wake katika bao la kwanza, akisema pasi yake ilikuwa muhimu.
“Niliuona mpira ule kutoka kwa Rashford, ulikuwa krosi nzuri sana kwa mshambuliaji. Kwangu ni muhimu kupata mipira ndani ya boksi,” amesema Lewandowski.
Ameongeza kuwa ushindi huo haukuwa rahisi: “Nina furaha kufunga bao muhimu na kushinda. Tulilazimika kupambana hadi mwisho. Kabla ya mechi tulijua kushinda hapa si rahisi.”
Lewandowski pia alikiri timu yao haikuwa bora kipindi cha kwanza: “Tulicheza taratibu sana kipindi cha kwanza, lakini tuliboresha zaidi katika kipindi cha pili.”
Kwa ushindi huo, Barcelona imeendelea kujiweka katika nafasi nzuri ya kutetea ubingwa wao, huku sasa macho yakielekezwa katika kufikia rekodi ya pointi 100, mafanikio ambayo yatakuwa alama kubwa katika historia ya klabu hiyo.