Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Matokeo mabaya, yaweka rehani nafasi ya tano ya EPL UCL

Muktasari:

  • Manchester City ilichapika kwa mabao 3-0 dhidi ya Real Madrid, Chelsea ikapoteza 5-2 dhidi ya PSG, huku Arsenal ikiambulia sare ya bao 1-1 na Bayer Leverkusen.

LONDON, ENGLAND: KATIKATI ya wiki hii, matumaini ya Ligi Kuu England (EPL), kupata nafasi tano za moja kwa moja kufuzu katika Ligi ya Mabingwa Ulaya yamepata changamoto baada ya matokeo mabaya ya timu za ligi hiyo katika mashindano ya Ulaya.

Manchester City ilichapika kwa mabao 3-0 dhidi ya Real Madrid, Chelsea ikapoteza 5-2 dhidi ya PSG, huku Arsenal ikiambulia sare ya bao 1-1 na Bayer Leverkusen.

Tottenham Hotspur pia ilipoteza kwa mabao 5-2 dhidi ya Atletico Madrid, Liverpool ikapoteza 1-0 dhidi ya Galatasaray SK na Newcastle United ikatoka sare ya mabao 1-1 nyumbani dhidi ya Barcelona. Hali hii imeongeza shinikizo kubwa na hatari ya kutoingiza timu tano kwa England, ambazo mara nyingi huamuliwa na viwango vya timu za ligi husika.

Msimu uliopita, Newcastle United ilikuwa timu ya tano kufuzu Ligi ya Mabingwa Ulaya licha ya kumaliza ligi katika nafasi ya tano.

Hiyo ilitokana na ukweli kwamba Shirikisho La Soka Ulaya (UEFA) hutumia mfumo maalumu wa UEFA coefficient, ambapo kila ligi hujikusanyia pointi kwa kufanya vizuri na msimu ukimalizika, wakati ligi husika ikiwa na pointi nyingi inapewa nafasi ya kupeleka timu tano.

Kwa sasa England bado inaongoza katika msimamo ikiwa na pointi 22.513, ambazo ni pointi 4.5 mbele ya Spain iliyo katika nafasi ya pili na pointi 18.031, huku Ujerumani ikiwa ya tatu kwa pointi 18.000.

Hata hivyo, kwa kuwa mechi za Manchester City, Chelsea na Tottenham Hotspur hazionekani kuwa nzuri na huenda timu hizo zikatolewa, itahitajika nguvu ya ziada ili kusaidia ligi hiyo kutoshushwa.

Kila ushindi katika mashindano ya Ulaya unalipwa pointi mbili, sare pointi moja, huku pia kukiwa na pointi za ziada kwa kupita hatua za mtoano ambapo huwa ni pointi 1.5 katika Ligi ya Mabingwa Ulaya, 1 katika UEFA Europa League na 0.5 kwenye UEFA Europa Conference League.

Kwa msimu huu, matokeo ya Aston Villa dhidi ya Lille OSC, Nottingham Forest dhidi ya FC Midtjylland na Crystal Palace dhidi ya AEK Larnaca, ikiwa zitashindwa kwenye michuano mingine ya Europa na Conference, itakuwa muhimu sana kwa England kushikilia nafasi ya kwanza.

Baada ya awamu ya ligi ambapo timu tano za England katika Ligi ya Mabingwa Ulaya zilishika katika nafasi nane za juu na Aston Villa kumaliza nafasi ya pili katika UEFA Europa League, ilionekana kuwa nafasi ya ligi hiyo kuingiza timu tano ipo salama.

Hata hivyo, matokeo mabaya ya wiki hii yameweka shinikizo zaidi na matumaini pekee yalibaki kwa Villa, Forest na Palace zilizocheza mechi za michuano ya Europa na Conference, jana.